02 September 2013

KITENGO CHAWATEJA WAKUBWA CHAZINDULIWA



Na Mwandishi Wetu
BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imezindua huduma mpya itakayowapa nafasi wateja binafsi wakubwa kupata huduma mbalimbali na kutimiza malengo yao.Kitengo cha huduma hiyo iliyozinduliwa mwishoni mwa wiki kipo katika jengo la Coco Plaza, jijini Dar es Salaam, na kitafahamika kama Kitengo cha Huduma Binafsi za Kibenki kwa Wateja Wakubwa.

Akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi huo, Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF), Dk. Reginald Mengi, alisema huduma hiyo imekuja kipindi muhimu wakati Tanzania ikijizatiti kiuchumi."Wakati nchi yetu ikikua kiuchumi, mchango mkubwa sana unatolewa na taasisi za kibenki kama NBC. Idadi ya watu wanaohitaji huduma za kifedha inaongezeka kila kukicha," alisema.
Alisema kwamba huduma hii ya kisasa ni ya muhimu sana ikisisitiziwa na ukweli kuwa mashirika na makampuni yaliyofanikiwa kibiashara ni yale yaliyofanikiwa kubadili mifumo ya kibiashara kutokana na mazingira ya soka kwa manufaa ya wateja wao.
Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, mama Mizinga Melu alisema kwa miaka 46 ya NBC nchini, benki hiyo imekuwa ikiendelea kuongeza idadi ya wateja kutoka kila kada ya maisha wakiwa na mahitaji mapya na tofauti.
"Ni kutokana na hilo ndio maana tumeamua kuanzisha Huduma Binafsi za Kibenki kwa Wateja Wakubwa ambapo kitengo chake kitakuwa kikitoa huduma kutokana na mahitaji maalumu," alisema.Mama Melu alisisitiza kwamba NBC hufanya kila liwezekanalo kuwaandalia wateja wake mazingira bora ya kuhudumia waweze kufikia malengo yao kirahisi.Ili mteja aweze kujiunga na Huduma Binafsi za Kibenki kwa Wateja Wakubwa kutoka NBC atapaswa kuwa na kipato au mshahara usiopungua shilingi milioni 7.5 kwa mwezi..

No comments:

Post a Comment