20 August 2013

YANGA YAPATA PIGO



 Na Amina Athumani
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara Yanga, imeanza kukumbwa na majeruhi katika kikosi chake ambapo jumla ya wachezaji watano jana walishindwa kufanya mazoezi kutokana na kuumia.Wachezaji hao ni Simon Msuva, Kelvin Yondani, Mbuyu Twite, Ally Mustapha 'Barthez' na Mrisho Ngassa

Akizungumza Dar es Salaam jana, wakati wa mazoezi ya timu hiyo yanayofanyika katika shule ya Loyola Mabibo,Dar es Salaam, Daktari wa timu hiyo Nasoro, Matuzya alisema wachezaji hao kila mmoja anasumbuliwa na majeraha yake.Alisema kwa upande wa Twite ambaye aliumia na kushonwa nyuzi tatu mdomoni, jana alijaribu kuingia mazoezini lakini alishindwa kuendelea baada ya kupata maumivu makali kichwani .
Alisema Ngassa anasumbuliwa na kichwa huku mchezaji Yondani bado akiwa na maumivu ya mguu aliyoyapata katika mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Azam FC na Msuva alipata majeruhi katika mazoezi ya jana.
Alisema kutokana na hali zao mwalimu hatawaingiza mazoezini hadi hapo watakapopata nafuu na kwamba wanategemea hadi keshokutwa wachezaji hao watakuwa fiti kujiunga na wenzao kwa ajili ya maandalizi ya mechi za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.Katika pazia la Ligi Kuu Yanga wataanza kampeni zao za kutetea taji hilo kwa kucheza na Ashanti United.

No comments:

Post a Comment