Na Daud Magesa, Mwanza
WIZARA ya Maliasili na Utalii, Idara ya
Wanyamapori kwa kutumia wataalamu wake, inafanya ziara ya kutembelea na kutoa
elimu kwenye maeneo yenye matatizo ya fisi wanaoua watu hasa watoto wadogo
katika vijiji vya Masemele na Chabakima katika mikoa ya Mwanza na Geita.
Akizungumza na
gazeti hili jana mwakilishi wa wizara hiyo,Twaha Twaibu alisema ziara hiyo
imelenga kubaini chanzo cha tatizo na kutoa elimu kwa wananchi kwa njia ya
mikutano pamoja na kuwaonesha sinema za wanyamapori kuhusu tabia za wanyama hao
ambayo itahitimishwa Agosti 25, mwaka huu .
Alisema
kutokana na kuongezeka kwa matukio ya wanyamapori kushambulia na kuua binadamu
hasa watoto wadogo kwenye maeneo mengi ya Mkoa wa Mwanza, Geita na
Simiyu,Wizara imewatuma wataalamu hao kuelimisha wananchi kuhusiana na kadhia
hiyo
Bw.Twaha Twaibu
ambaye ni Mkuu wa Uenezi wa Idara ya Wanyamapori Dar es Salaam pamoja na
Benjamini Kijika ambaye ni mkuu wa kikosi dhidi ya ujangili Kanda ya Ziwa
wamesema kuwa Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali, ambapo kwa kipindi
cha mwaka jana na hadi sasa jumla ya fisi 11 wameuawa na kikosi hicho.
Bw.Twaibu alisema kwa baadhi ya
wananchi waliopata matatizo wizara iliweza kuwalipa na inaendelea na mchakato
wa kuwalipa wananchi wengine waliopatiwa na matatizo.
Alisema katika kipindi cha mwaka
2012/13 pekee kufikia Juni,2013, familia 93 zililipwa kifuta machozi cha sh.
49,200,000 kwa wananchi waliojeruhiwa na wanyama wakali wakiwemo fisi kwa nchi
nzima.
Akiwa katika vijiji vya Masemele na
Chabakima, Twaibu alitoa pole kwa familia zilizopoteza ndugu katika ziara hiyo
iliyoanza jana, kwenye vijiji vya Masemele na Chabakima, katika kata ya Bugogwa
katika Wilaya ya Ilemela, Mkoa wa Mwanza na itaendelea katika maeneo mengine
kama Wilaya za Magu na Geita.
"Kwa niaba ya Wizara ya Maliasili
na Utalii na Serikali ,ninawapa pole familia za wananchi wote wa Mikoa ya Kanda
ya Ziwa kwa matatizo yaliyowapata ya kujeruhiwa au kupoteza ndugu zao
wapendwa.Wizara imekuwa ikitoa kifuta machozi kwa kuwalipa wananchi
waliojeruhiwa na kuuawa na wanyamapori wakali wakiwepo fisi na itaendelea
kufanya hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 71 cha Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori
Na.5 ya mwaka 2009," alisema Twaibu.
Bw.Benjamini Kijika aliwaeleza wananchi
hao kuwa suala la kusaka fisi limekuwa na vikwazo ambavyo yeye kama mtaalamu
wameshindwa kuelewa na kuhisi kuna masuala ya ushirikina kuhusu fisi hao.
Alisema alipoitwa na kuelezwa kuwa fisi
wameonekana kijijini na kufanya msako, wanyama hao hawakuonekana wala kusikia
sauti ya wanyama hao hata walipofuatilia zaidi hawakufanikiwa kuwaona na wakati
mwingine waliwahi kuelezwa na wananchi Wilaya ya Ilemela kijiji cha Muhonzi
kuwa fisi ameua mtoto wa shule na wananchi walimsaka na kumuua fisi huyo.
Hata hivyo alidai kushangazwa mara
baada ya askari wanyamapori kufika eneo la tukio hawakuona dalili zozote za
damu wala mikwaruzo ya alama ya mtoto na nyayo za fisi, isipokuwa waliona nguo
za mtoto huyo aliyekamatwa na fisi zikiwa zimetundikwa juu ya mti zikiwa hazina
hata damu wala kuchanwa, kitu ambacho ni tofauti na tabia za mnyama huyo
anaposhambulia binadamu.
Kijika aliwaomba wananchi kusaidia
kukabiliana na tatizo hilo na inawezekana vipo vitendo vya ushirikina
vinafanyika, na kama vipo waviache.
Hivi karibuni gazeti
la Mzawa toleo la Agosti 17 mwaka huu,lilikuwa na kichwa cha habari 'Fisi
wahusishwa na Ushirikina Bariadi', likieleza jinsi jeshi la Sungusungu la
kijiji cha Ng'hesha walivyolazimika kuwacharaza viboko akinamama vikongwe,
wakitaka kubaini chanzo cha matukio hayo.
No comments:
Post a Comment