12 August 2013

YANGA NAO WAIFANYIA KWELI SC VILLA

  • YAIFYATUA MABAO 4-1 TAIFA


Na Elizabeth Mayemba
MABINGWA wa Tanzania Bara, Yanga jana walidhihirisha kwamba ni mabingwa wa kweli, baada ya kuinyuka SC Villa ya Uganda mabao 4-1, katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam

Waganda hao juzi pia walipokea kichapo cha mabao kama hayo kutoka kwa Simba katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa katika uwanja huo huku 'Wekundu' wakiadhimisha siku yao ya 'Simba Day' inayofanyika kila mwaka.
Mpira ulianza kwa kasi kwa timu zote kushambuliana lakini, Yanga ndiyo ilianza kupata bao la kwanza dakika ya saba lililokwamishwa kimiani na Mrisho Ngassa, kwa shuti la mbali lililomshinda kipa wa SC Villa, Elungat Martin.
Villa ilisawazisha bao hilo dakika ya 18 kupitia kwa Siraj Jamal, baada ya kutokea piga nikupige langoni mwa Yanga huku mabeki wake wakishindwa kuokoa hatari hiyo.
Nadir Haroub 'Canavaro' aliipatia Yanga bao la pili dakika ya 27, baada ya kuachia shuti la mbali baada ya kupokea pasi fupi ya Haruna Niyonzima aliyepiga mpira wa faulo langoni mwa Villa.
Yanga iliendelea kuliandama lango la wapinzani wao ambapo mshambuliaji, Didier Kavumbagu aliwapatia mabingwa hao wa Tanzania Bara bao la tatu dakika ya 30 akimalizia shuti lililopigwa na Jerry Tegete, lililogonga mwamba wa lango la Villa na kumkuta mfungaji.
Katika kipindi hicho Villa ambayo juzi ilinyukwa mabao 4-1 na Simba, walizidiwa kila idara na kuruhusu washambuliaji wa Yanga, kulitia misukosuko lango lao mara kwa mara.
Kipindi cha pili Yanga, waliingia kwa kasi huku Kavumbagu akikosa bao dakika ya 50, baada ya kuachia shuti kali lililotoka nje kidogo ya lango la Villa.
Yanga iliongeza bao la nne dakika ya 61 lililopachikwa na Niyonzima, aliyetoka na mpira katikati ya uwanja na kuachia shuti lililotinga moja kwa moja wavuni.

No comments:

Post a Comment