13 August 2013

WAPANDA JUU YA MTI KUPIGA SIMU



Na Steven William, Muheza
WANANCHI wa Kijiji cha Kwelumbizi Kata ya Zirai Tarafa ya Amani wilayani Muheza wameiomba Serikali kuzishawishi kampuni za simu za mkononi kujenga minara katika kijiji hicho cha Kwelumbizi ili wananchi wapate mawasiliano ya uhakika kwani kwa sasa wanapata shida.

Wananchi hao walisema kwa muda mrefu sasa wamekuwa wakipata tabu ya mawasiliano kutokana na kutokuwepo minara ya mawasiliano hivyo kuzidi kuwarudisha nyuma katika harakati za maendeleo.
Mmoja wa wakazi wa kijiji hicho, Tekra Jemes Makundi alisema kuwa kwa sasa wakitaka kuwasiliana na watu huko mjini mpaka wapande juu ya miti mirefu ndiyo wanapata mawasiliano kupitia mnara kutoka Maramba wilayani Mkinga.
Alisema kuwa kutokana na hilo tayari baadhi ya watu wameshaanguka na kuvunja miguu kwa ajili ya kutafuta mawasiliano juu ya miti, Makundi ambaye ni mfanyabiashara wa kukusanya iliki na mdalasini alisema kuwa wanamuomba Waziri wa Mawasiliano kuzishawishi kampuni za simu kujenga mnara katika kijiji hicho kwa kuwa kina watu wengi wanaomiliki simu na kinawafanyabiashara wengi.
Nae Mwenyekiti wa Kijiji cha Kwelumbizi, Shabani Kipala alisema kuwa wameweza kuleta maendeleo ndani ya kijiji hicho kwa kujenga shule ya sekondari ya kata ya Zirai na kuomba serikali kuongeza walimu shuleni hapo

No comments:

Post a Comment