Na Rachel
Balama
MAHAKAMA ya Hakimu
Mkazi Kisutu Dar es Salaam, amewahukumu kifungo cha miaka mitatu jela kila
mmoja wafanyabiashara wawili baada ya kukiri kukamatwa na kilo 6.5 za madini ya
urani.Hukumu
hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Geni Dudu.
Wafanyabiashara hao ni Duncun Mwakanemela (41), mkazi wa Ubungo NHC na Sylivia
Anania (42), mkazi wa Manzese ambao wanadaiwa kutenda kosa hilo Septemba 6,2012
katika maeneo ya Ubungo na Manzese.
Wakili
wa Serikali, Charles Anindo, aliiomba mahakama hiyo itoe adhabu kali kwa
washtakiwa kutokana na madini hayo kuwa na madhara makubwa yanapokuwa mikononi
mwa watu ambao hawana leseni wala utaalamu wa kuyatunza.Baada
ya ombi hilo, Hakimu Dudu alimuuliza mshtakiwa Mwakanemela kama ana lolote la
kuieleza mahakama hiyo ili iweze kumpunguzia adhabu.
Mwakanemela
aliiomba mahakama imsamehe akidai anasumbuliwa na shinikizo la damu,
anategemewa na mama yake ambaye ni mzee sana na aliyapata madini hayo kwa
mshtakiwa mwenzake Anania bila kujua kama ni hatari."Mheshimiwa
Hakimu sikujua kama madini haya ni hatari ndiyo maana nilikuwa nakaa nayo
ndani... wakati Anania ananipa alisema ni dawa ya mahindi ili nitafute soko
ndiyo maana nikayaweka ndani," alisema.
Kwa
upande wake, Anania aliiomba mahakama imsamehe kwa kosa alilotenda na
kumpunguzia adhabu.Alisema
yeye alipelekewa madini hayo hatari na mtu anayeitwa James ambaye walifahamiana
miezi sita iliyopita baada ya kumwambia ni dawa ya mahindi."Mheshimiwa
Hakimu baada ya kupewa mzigo huo, nilikaa nao ndani na niliuweka pembeni ya
kitanda changu kwa sababu sikujua kama ni madini hatari yenye madhara.
Baada
ya washtakiwa kutiwa hatiani, Hakimu Dudu alisema adhabu ya kifungo cha miaka
mitatu jela imezingatia kifungu cha 11(1) na (2) cha sheria ya nguvu za Atomic
(mionzi), namba 7 ya mwaka 2004.
Alisema
washtakiwa wamefanya kosa hilo kwa mara ya kwanza hivyo mahakama imezingatia
utetezi walioutoa kwani madini hayo yana mionzi ambayo ni hatari kwa viumbe
hai.
"Sheria hii
inasema mtu akikamatwa lazima alipe faini ya sh. milioni tatu au kifungo cha
miaka mitatu jela... nimelazimika kutoa adhabu hii kwa sababu mlikuwa hamjui
madhara yake.
"Kwa sababu
hatujui mmekaa na madini haya muda gani, Ofisa Jamii awaangalie ndani ya siku
14 mkiwa gerezani na ajiridhishe kama mmeathirika na mionzi ili aifahamishe
Serikali muweze kutumikia kifungo cha nje," alisema Hakimu Dudu.
Akitoa ushahidi wake
mahakamani hapo, mtaalamu kutoka Tume ya Nguvu za Mionzi, mkoani Arusha, Bw.
Leonard Daniel, alisema madini hayo yana madhara makubwa kwa viumbe hai na
hayapaswi kuwekwa karibu na watu bila ya kufunikwa kitaalamu.
Alisema madini yaliyokamatwa yanaweza kuleta madhara kwa mtu yeyote
aliyeyakaribia katika muda wa miaka mitatu hadi sita kwa kuzaa mtoto mlemavu,
kuathirika viungo vya ndani kama ini, figo, mapafu na kubadilisha mfumo wa
uzazi
No comments:
Post a Comment