07 August 2013

UFISADI HALMASHAURI



  • WATENDAJI WATUHUMIWA KUTAFUNA MAMILIONI YA KODI MIAKA 30
  • MADIWANI,DED WASHANGAA  FEDHA ZILIKO WAUNDA TUME MAALUM

Na Mwandishi Wetu, Mbozi
MAMILIONI ya fedha za Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya yanayotokana na pango la nyumba tatu za halmashauri hiyo yanadaiwa kutafunwa na watendaji kwa miaka 30 iliyopita.watendaji wanatuhumiwa kuficha vyanzo vya mapato hayo kwa nia ya kujinufaisha wenyewe.

Hoja hiyo iliibuliwa mwishoni mwa wiki katika kikao cha Baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo na Diwani wa Kata ya Ihanda, Joel Kasebele (CCM) wakati wa maswali ya papo kwa papo kwa Mkurugenzi wa halmashauri, Levison Chilewa ambaye alitakiwa kutoa ufafanuzi juu ya mahali zinapokwenda fedha za pango za nyumba tatu.
Diwani huyo alisema, nyumba hizo zimepangishiwa watu na taasisi binafsi za Tanganyika Farmers Association (TFA), Chama cha Akiba na Mikopo karibu na soko la Vwawa na nyumba ya kulala wageni ya Mbozi Development Council (MDC) ambazo tangu zilipopangishwa mwaka 1983 hakuna mapato yaliyoingizwa kwenye halmashauri hiyo.
"Mheshimiwa Mwenyekiti napenda kupata ufafanuzi juu ya mapato ya fedha zinazotokana na nyumba tatu zinazomilikiwa na halmashauri yetu, zinakwenda wapi? Nyumba hizo ni za halmashauri mapato yake yanafanya kazi gani?” alihoji Kasebele.
Akijibu hoja hiyo, Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Chilewa alisema kuwa hajui fedha za nyumba hizo zinakokwenda na kwamba tangu ameingia hapo miaka saba iliyopita hajawahi kupewa taarifa kuhusu mapato ya nyumba hizo na kwamba hata hivyo ofisi yake imewaandikia barua wapangaji ili kujua mkataba wa upangaji wa nyumba hizo.
"Lazima niseme ukweli hili jambo nimelikuta, sijui lolote kuhusu mapato ya nyumba hizo, tangu nimefika miaka saba sasa sijapewa mrejesho wowote kuhusu nyumba hizo," alisema Chilewa.
Kufuatia majibu hayo baadhi ya madiwani walisimama ili kupata ufafanuzi zaidi na kuhoji sababu za ofisi ya halmashauri hiyo kuachia mapato ya nyumba hizo kwa takriban miaka 30 bila kufuatiliwa.
Alisema kuwa, siku za nyuma hakukuwa na kumbukumbu wala taratibu zozote za vyanzo vya mapato kutoka kwa uongozi uliopita na kwamba nyumba hizo zimeibuliwa hivi karibuni ambapo jitihada zinafanyika ili kujua mikataba ya wapangaji.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Elick Ambakisye alisema kuwa kikao cha Baraza la Madiwani kimeiagiza ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuandaa taarifa sahihi ya kina juu ya vyanzo vingine vya mapato ambavyo fedha zake zinaingia mifukoni mwa wachache.
Mwenyekiti huyo alisema, wanasubiria kutoa uamuzi wao juu ya kinachoendelea kuhusiana na tukio hilo katika kikao cha Baraza la Madiwani kinachotarajiwa kukutana Agosti 14, mwaka huu.
Hata hivyo, awali ilidaiwa kuwa, baadhi ya watendaji wa halmashauri hiyo wamekuwa wakichukua kodi katika nyumba tatu za halmashauri hiyo bila kuziwasilisha ofisini huku wengine wakijimilikisha nyumba hizo na kufahamika kwa wapangaji kama ni wamiliki wa nyumba hizo.
Wakati huo huo, jitihada za kuwatafuta wapangaji wa nyumba hizo ili kupata taarifa za kodi wanazolipa kila mwezi zinaendelea baada kufuatiliwa muda mrefu bila mafanikio.

1 comment:

  1. MIAKA THELASINI MULIKUWA WAPI JE NI KUONYESHA IWAPO MUNAFANYA KAZI MUTAPIMWA UCHAGUZI UJAO IWAPO MUTAGOMBEA KWA KATIBA MPYA

    ReplyDelete