Na Darlin Said
WAZIRI Mkuu mstaafu,
Bw. Frederick Sumaye, amesema Rasimu ya Katiba Mpya imeshindwa kuonesha
msisitizo wa kutatua matatizo ya rushwa, ufisadi, dawa za kulevya ambayo
husababisha Watanzania wakose imani na Serikali yao.Bw. Sumaye aliyasema
hayo Dar es Salaam jana wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Katiba la
Shirikisho la Vyama Huru vya Wafanyakazi nchini (TUCTA), ambao ulijadili Rasimu
ya Katiba Mpya
.Alisema bila
kuyadhibiti madhambi hayo katika nchi, Katiba hata iwe nzuri kiasi gani itakuwa
kazi bure ambapo wananchi hawataona manufaa ya katiba hiyo, matunda ya juhudi
zao.Aliongeza kuwa,
ingawa rasimu hiyo ni nzuri ila bado haijagusa mambo hayo ambayo yanawatesa
watu kama rushwa ambayo inahatarisha amani ya nchi.
"Kulingana na
ukubwa wa matatizo haya kwa amani ya nchi na ukuaji wa uchumi, natamani rasimu
hii ingetaja kipengele cha kuundwa Mahakama Maalumu ya makosa hayo na iruhusu
adhabu kali kwa wahusika," alisema Bw. SumayeAkizungumzia ufisadi,
Bw. Sumaye alisema tatizo hilo ni kubwa ambalo linahujumu uchumi wa nchi hivyo
kuwakatisha tamaa wananchi kutokana na ongezeko la ugumu wa maisha.
Alisema tatizo la
dawa za kulevya, pamoja na kuwaathiri zaidi vijana, pia linasababisha kushusha
heshima ya Tanzania na kuvitaja vipengele alivyodai vina utata likiwemo suala
la Muungano."Ni vyema
tukaainisha changamoto zilizokuwepo katika mfumo wa Serikali mbili na kuzipatia
ufumbuzi wake...kama tutashindwa kupata ufumbuzi, mivutano hiyo itaendelea
kuwepo katika Serikali tatu na zitatokea changamoto nyingine hasa katika
Serikali ya Muungano na ile ya Tanganyika," alisema.
Aliyataja maeneo
mengine yanayopaswa kujadiliwa kuwa ni suala la Makamu wa Rais kushika madaraka
kama rais atafariki na kudai kuwa, huo ni mfumo mbovu kwa sababu rais lazima
achaguliwe na kama atakufa kutasababisha minong'ono hata kama Makamu wa Rais
hausiki na kifo chake.
"Rasimu haielewi
uwiano utakuwa wa namna gani, kama hakutakuwa na ufafanuzi kunaweza kutokea
usumbufu katika Muungano...eneo lingine ni lile la mapato lazima ielezwe
wazi," alisema Bw. Sumaye.
Madaraka ya Rais
Bw. Sumaye alisema,
kuna maeneo mengine ambayo watu wameyatolea maoni hasa suala la madaraka ya
rais jambo ambalo hata yeye anaamini baadhi ya nafasi anazoteua kiongozi wa
nchi zinapaswa kuthibitishwa na vyombo vingine kama Bunge au chombo kingine kwa
mujibu wa katiba husika.
Alisema hiyo
haimpunguzii rais madaraka bali inamsaidia na kumkinga. "Jambo hili
linafanyika katika nchi nyingi sioni kwanini liwe na shida kwetu hivyo
liangaliwe," alisema.
Naye kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bw. Kingunge Ngombalemwilu,
aliwataka viongozi kuwa waadilifu na wafuate sheria ili kuepusha matatizo
yanayoibuka hivi sasa na kujenga maisha ya wananchi.
.
.
No comments:
Post a Comment