06 August 2013

SERKALI YAAGIZA WATOTO WAENDE SHULE


NAIBU Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Aggrey Mwanri ameagiza watoto wote kwenye shule za msingi ni lazima waende shule.Alisema hata kama hawana fedha za michango ama sare waruhusiwe kuvaa nguo za kawaida huku akiagiza suala la michango ni la wazazi sio wanafunzi.

Aliyasema hayo juzi wakati anahutubia wananchi kwenye mji wa Chanika uliopo Halmashauri ya Mji Handeni ambapo alisema kitendo cha kuwarudisha watoto nyumbani kutokana na michango mbalimbali kuna baadhi ya wazazi wanafurahia hasa wenye watoto wa kike.
"Watoto waende shuleni hata kama wamevaa pensi nyanya. Na pia kutokutoa ada au michango sio suala la mtoto bali mzazi. Hivyo vita ya kudai michango ifanywe kwa wazazi walioshindwa kulipa michango hiyo.
"Kitendo cha kumrudisha mtoto nyumbani akikutana na wazazi wasiopenda watoto wao kusoma na kama ni mtoto wa kike, atafurahia kwa vile atakuwa amepata binti wa kuozesha. Au nyinyi hamjasikia kuna wazazi wanawalaumu watoto wao waliofaulu. Mzazi anamwambia mtoto si unaona nilikwambia usifanye vizuri, unaona sasa umefaulu," alisema Mwanri.
Akizungumza kwenye mkutano wa majumuisho baada ya ziara ya siku mbili kwenye Halmashauri ya Wilaya na ile ya Mji wa Handeni, Mwanri aliwataka watumishi kuwasikiliza wananchi na kumaliza kero zao badala ya kuwachenga na kwenda kunywa supu ama kubishana mambo ya mpira.
"Hakuna kitu kinawakera wananchi kama kutosikilizwa matatizo yao...wewe muda wote upo kwenye 'Pub' unapiga supu, ukifika ofisini unabishana mambo ya Simba na Yanga," alisema Mwanri.
Mwanri ameagiza majengo yote ya Serikali yanayojengwa nchini yawe na mifumo ya maji na umeme ni baada ya kukuta baadhi ya majengo kwenye Wilaya ya Handeni yakiwa hayana mifumo hiyo na kusema majengo hayo ikiwemo zahanati na nyumba za walimu haziwezi kukaa milele bila kuwekwa umeme.
Akisoma taarifa, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Thomas Mzinga alisema halmashauri yao ambayo ni mpya inakabiliwa na matatizo mbalimbali ikiwemo miundombinu ya maji na uchakavu wa mitambo kwenye Mji wa Handeni na kuungua mara kwa mara kwa mota za pampu za kusukuma maji.
"Pia tuna uhaba wa ofisi kwa baadhi ya maofisa kama vile mwanasheria, idara ya elimu na sekondari, maji, ardhi, maliasili na mazingira na ofisa manunuzi, uhaba wa fenicha elimu ya msingi na sekondari, afya, huku tukiwa hatuna ukumbi wa mikutano, uhaba wa usafiri na vitendea kazi. Na Halmashauri ya Mji iliomba fedha za kujenga ofisi kuu lakini ombi halikupita," alisema Mzinga

No comments:

Post a Comment