05 August 2013

RAIS SHEIN ATETA NA CLINTON


Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
RAI S wa Za n z i b a r n a Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali anayoiongoza ni kuhakikisha huduma muhimu za afya zikiwemo kinga na tiba zinapatikana kwa urahisi kwa wananchi wote.



Akizungumza na Rais Mstaafu wa Marekani, Bill Clinton ofisini kwake Ikulu jana, Dkt. Shein alisema Zanzibar imepiga hatua katika utoaji huduma za kinga na tiba kwa wananchi wake lakini changamoto inayokabiliana nayo ni namna ya kuyafanya mafanikio hayo kuwa endelevu.
"Tumepata mafanikio katika kinga na tiba kama vile malaria na vifo vya watoto wachanga lakini changamoto inayotukabili ni mafanikio haya kuwa endelevu," alieleza Dkt. Shein.
Hata hivyo Rais alibainisha kuwa pamoja na kujivunia mafanikio hayo anatambua kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya jitihada za pamoja kati ya Serikali na washirika wake wa maendeleo ukiwemo Mpango wa Upatikanaji Huduma za Afya wa Clinton (Clinton Health Access Initiative-CHAI) ulio chini ya Taasisi ya Clinton (Clinton Foundation).
"Baadhi ya wenzetu (nchi nyingine) huja kujifunza kujua tumepata vipi mafanikio haya lakini sisi tunatambua kuwa ni matokeo ya jitihada za pamoja na washirika wetu mkiwemo nyinyi (Clinton Foundation) hivyo hatuna budi kueleza shukrani zetu kwenu kwa kutuunga mkono," alisema Dkt. Shein.
Aliipongeza taasisi hiyo kwa jitihada zake za kusaidia kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa nchini zinazoendelea ambapo kwa Zanzibar taasisi hiyo imekuwa ikisaidia katika kuimarisha huduma za uchunguzi wa magonjwa, huduma kwa watu wenye virusi na ugonjwa wa UKIMWI, kifua kikuu pamoja na tiba na kinga ya ugonjwa wa malaria.
Kwa hivyo Dkt. Shein amemueleza Bw. Clinton kuwa anaamini jitihada zinazofanywa na Serikali yake pamoja na kuunganisha nguvu za washirika wa maendeleo mafanikio zaidi yatapatikana.
"Tunaanzisha Taasisi ya Tiba katika Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA) ili kufundisha madaktari hapa nchini huku watumishi wengine wa afya wakipata mafunzo katika Chuo cha Afya hapa hapa," alifafanua.
Aliongeza kuwa kwa kufanya hivyo nchi itakuwa na wataalamu wa afya wa kutosha na watasambazwa maeneo ya vijijini hivyo suala la uhaba wa watumishi hao litakuwa limepungua kama si kwisha kabisa.
Dkt. Shein alimhakikishia Bw Clinton kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kushirikiana na washirika wa maendeleo pamoja na mashirika ya kujitolea kama Clinton Foundation katika kuimarisha utoaji huduma mbalimbali kwa wananchi.
"Napenda nikuhakikishie Serikali yangu imedhamiria kuwapatia wananchi huduma za afya na nyinginezo na tuko tayari kuendelea kushirikiana na washirika wetu katika kufikia azma hii," alisema.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein alitumia fursa hiyo kueleza uhusiano mzuri uliopo kati ya Serikali na wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Marekani.
"Uh u s i a n o wa Ta n z a n i a na Marekani ni mzuri sana na umethibitishwa na ziara za mara kwa mara za viongozi wa nchi zetu," alisema Dkt. Shein na kutolea mfano ziara ya Rais Obama iliyofanyika nchini Tanzania hivi karibuni.
Kwa upande wake Rais Mstaafu wa Marekani, Bw. Bill Clinton amemwambia Rais wa Zanzibar kuwa amefurahi kuwa taasisi yake imepata fursa ya kutoa mchango wa kuimarisha utoaji huduma za afya kwa wananchi wa Zanzibar.
Rais huyo Mstaafu wa Marekani ambaye amefuatana na binti yake Chalsea yupo nchini ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya nchi tano barani Afrika kukagua miradi iliyo chini ya ufadhili wa taasisi yake hiyo. Nchi nyingine ni Malawi, Zambia, Rwanda na Afrika Kusini.
"Zanzibar ni sehemu ya Jumuiya ya Kimataifa inayounga mkono jitihada na kazi za taasisi yetu hivyo nimefurahi kufika kwangu hapa leo," alibainisha Bw. Clinton.
Viongozi wengine waliohudhuria mazungumzo hayo ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Dkt. Mwinyihaji Makame na Waziri wa Afya Juma Duni Haji na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Mohamed Saleh Jidawi.  

No comments:

Post a Comment