05 August 2013

KIKWETE AKUTANA NA BINGWA WA KURUKA KAMBA


Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete juzi amekutana na mtoto wa Kitanzania ambaye ni Bingwa wa Dunia wa mchezo wa kuruka kamba, Hamisi Kondo mwenye umri wa miaka 14.Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Kurugenzi ya Mawasiliano ya Ikulu, mbali na kukutana na Rais, Kondo na wenzake pia walifanya maonesho ya mchezo huo kwa Kikwete ambaye amefurahishwa na vipaji vya watoto hao wa Kitanzania
.Taarifa hiyo ilieleza kuwa Rais Kikwete amekutana, na Kondo pamoja na washiriki wengine waliounda timu ya Tanzania iliyoshiriki katika Michuano ya Dunia ya Kuruka Kamba iliyofanyika Florida, Marekani kati ya Julai 5 hadi 13, mwaka huu ambapo nchi 14 zilishiriki.Mbali na Tanzania, nchi nyingine zilizowakilisha Bara la Afrika katika mashindano hayo ni Afrika Kusini na Kenya. Miongoni mwa nchi nyingine duniani ziliwania medali katika michuano hiyo ya Dunia ni Marekani yenyewe, Canada, Ufaransa, Ujerumani, Mexico na Japan.
Kondo, ambaye alilelewa kwa muda katika Kituo cha Watoto Yatima cha Dogo Dogo Center cha Dar es Salaam, sasa anasoma katika Shule ya Msingi ya Seaside Catholic School, mjini Seattle, Jimbo la Washington ambako mwezi ujao anatarajiwa kuingia darasa la saba.
Mtoto huyo ambaye anaondoka nchini leo kurejea Marekani, aliondoka nchini mwaka jana baada ya kuwa ameonesha kipaji kikubwa katika mchezo wa kuruka kamba.
Kabla ya kwenda Marekani alikuwa ameshinda ubingwa wa Tanzania na ule wa Afrika Mashariki katika mashindano yaliyofanyika mwaka 2010 mjini Mombasa, Kenya.
Taarifa hiyo ilieleza kwamba kwenye ujumbe huo uliokutana na Rais Kikwete, alikuwepo pia Mama Amy Kennedy ambaye yeye pamoja na mume wake, Dennis Kennedy ndiyo wafadhili wakuu wa Kondo na wanamiliki moja ya sehemu bora zaidi za kufanyia mazoezi duniani.
"Ni wafadhili hao waliomtafutia Kondo shule kule Marekani na wanaendelea kulipia gharama za masomo yake, kugharamia mazoezi yake, kulipia gharama zake za usafiri kwenda kwenye mashindano mbalimbali," ilisomeka sehemu ya taarifa hiyo.
Wafadhili hao ndiyo waliisafirisha timu ya Tanzania, kwenda kushiriki katika mashindano hayo ya Marekani ambako pia walilipia chakula na malazi ya timu hiyo.

No comments:

Post a Comment