Na Gladness Mboma
JESHI la Polisi nchini limesema liko tayari muda wowote
kushirikiana na Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Ujenzi
(AQRB) ili kuhakikisha ujenzi wa majengo yote nchini unashirikisha wabunifu
majengo.
Sambamba na wakadiriaji ujenzi waliosajiliwa, wenye sifa stahili
ili kulinda usalama na mali za watumiaji. Kauli hiyo ilitolewa jana na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo
nchini, Paul Chagonja kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi, Said Mwema wakati
alipokuwa akimwakilisha katika mkutano wa pamoja kati ya jeshi hilo na bodi
hiyo.
Alisema kuwa, wanatambua majukumu ya AQRB kisheria hasa
kuwajibisha wataalamu na waendelezaji wa ujenzi wanaokiuka sheria na hata
sheria nyingine za nchi. "Ombi langu ni kuwa wale wanaokiuka sheria wawajibishwe na
bodi kwa mujibu wa sheria yenu na wale ambao wanatakiwa wapelekwe mahakamani
tushirikiane ili sheria ichukue mkondo wake," alisema.
Alisema kuwa, Jeshi la Polisi linashukuru kutambua dhamira ya
kuendeleza ujenzi wa makazi ya askari wao na kwamba wamekuwa wakiwatumia
wabunifu majengo, wakadiriaji ujenzi, wahandisi na makandarasi waliosajiliwa na
taasisi husika na wataendelea kuwatumia.
Chagonja alisema, kwa kufanya hivyo hata jamii haitaona jambo la
ajabu pale watakapokuwa wanachukua hatua za kisheria kwa wale ambao wanajenga
makazi yao bila ya kuwatumia wataalamu.
Alisema kuwa, wataendelea kuwatumia kikamilifu wabunifu majengo na
wakadiriaji majenzi ambao ni watumishi katika jeshi lake na kuwaendeleza wale
ambao hawajasajiliwa na bodi ili hatimaye wawe na sifa zinazotakiwa.
"Jambo muhimu tunaomba mtupatie ushirikiano wa karibu, hasa
pale ushahidi unatakiwa kutoka kwenu upatikane kwa muda mwafaka, ikumbukwe kila
fani ina wataalamu wake, hivyo ushirikiano wenu katika kutoa taarifa za
kitaalamu utasaidia sana wataalamu wa jeshi letu kuchukua hatua kwa wakati na
wepesi," alisema.
Chagonja alikiri kuwa, uelewa wa jamii kuhusu bodi na majukumu ya
wabunifu majengo na wakadiriaji majenzi ni mdogo sana na kwamba hata wao kama
sehemu ya jamii kuna baadhi yao hawafahamu majukumu ya bodi na yale ya
wataalamu.
"Hivyo dhamira yenu ya kujitangaza ni nzuri, kwani ndio njia
pekee ya kuwafanya wananchi watii sheria bila shuruti na kupunguza kesi
zinazotokana na watu kutenda mambo kwa mazoea bila kufuata
sheria,"alisema.
Naye Mwenyekiti wa bodi hiyo, Dkt. Ambwene Mwakyusa alisema lengo
la mkutano huo ni kujitambulisha kwa wadau wa kusimamia sheria kwa makosa ya
jinai ili kupanua uelewa wa majukumu ya bodi na pia umuhimu wa wataalamu
wanaowaratibu katika sekta ya ujenzi nchini.
Alisema, bodi ina jukumu la
kuingia na kukagua miradi ya ujenzi kwa lengo la kuhakikisha imebuniwa na
kusimamiwa na wataalamu waliosajiliwa na bodi, miradi ambayo imesambaa nchi
nzima kufikia Juni 30, mwaka huu ambapo bodi ilikuwa imesajili wataalamu 834 na
kampuni 276.
No comments:
Post a Comment