29 August 2013

BILIONI 4/- KUTUMIKA UJENZI WA CHUO KASULU



Na Respice Swetu, Kasulu
ZAIDI ya sh. bilioni nne zinatarajiwa kutumika kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi Nyamidaho kinachojengwa katika Tarafa ya Makere wilayani Kasulu Mkoa wa Kigoma.

Akizungumza juzi ofisini kwake, Ofisa Elimu Ufundi wilayani Kasulu, Gerard Nkona alisema, chuo hicho kinajengwa kutokana na msaada wa Shirika la Kimataifa la World Vision linalofanya shughuli zake wilayani humo.
Shirika hilo linalojishughulisha na utoaji wa huduma za kijamii kupitia miradi mbalimbali ya kimaendeleo nchini, tayari limetoa zaidi ya sh. bilioni 1.4 kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya kwanza ya ujenzi wa chuo hicho.
"Ambapo zaidi ya shilingi milioni tano, kati ya hizo zimetumika hadi sasa kwa kazi inayoendelea ya ujenzi wa jengo la utawala, madarasa na mabweni," alisema Ofisa huyo.
Pia alisema, chuo hicho baada ya kukamilika kitatumika kutoa mafunzo katika fani za ufundi umeme, seremala, uashi na sayansi kimu na baada ya hapo zitaongezwa fani zingine kadri ya maendeleo ya ujenzi wa chuo hicho ambacho kinatarajiwa kuwa kikubwa kuliko vyuo vya ufundi vilivyopo katika ukanda wa Magharibi mwa Tanzania.
Alifafanua pia kuwa, ujenzi wa chuo hicho ulioanza mwaka 2012 umepangwa kutekelezwa kwa awamu tatu huku ukitarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, mwaka 2014 lengo likiwa ni kupokea wanafunzi wa kujiunga na chuo hicho katika kipindi cha muhula wa masomo kitakachoanza mwezi Julai mwakani.
"Tunawashukuru wakazi wa Kijiji cha Nyamidaho kwa kukubali kutoa ardhi yenye ukubwa wa hekari 40 ili kupisha ujenzi wa chuo hicho na halmashauri ya wilaya ya Kasulu kwa kuchangia gharama za michoro," alisisitiza Nkona huku akitoa wito kwa vijana kuichangamkia fursa hiyo.
Hata hivyo, kujengwa kwa chuo hicho kunatarajiwa kuwa mkombozi kwa wakazi wa Wilaya ya Kasulu na maeneo jirani.

No comments:

Post a Comment