29 August 2013

MAKATIBU CCM KIKAANGONI



 Na Thomas Mtinge, Dodoma
MAKATIBU wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ngazi ya mikoa na wilaya nchini wameagizwa fedha zilizowekwa kwenye benki ya CRDB kwa ajili ya kuanzisha Family Benki, zirudishwe mara moja vinginevyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Agizo hilo lilitolewa mjini Dodoma juzi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa ya CCM, Abdallah Bulembo, ambapo alisisitiza kuwa hatua hiyo inatokana na kile alichodai kutoridhishwa kwake na mwenendo mzima wa kukusanya na kutunza fedha za kuanzisha benki hiyo kwa kuingia ubia na kampuni binafsi (jina tunalo).
Taarifa inaonesha kuwa akaunti hiyo ina sh. milioni 5 wakati fedha zinazodaiwa kukusanywa na makatibu hao ni zaidi ya s. milioni 20.
Bulembo alitoa agizo wakati akizungumza na Wajumbe wa Baraza Kuu la jumuiya hiyo katika kikao chake kilichofanyika Dodoma.
“Ndugu viongozi wenzangu mimi mpaka sasa sijaridhishwa kabisa na hatua zilizopo sasa za uanzishwaji wa benki hii. Binafsi napata shaka kubwa tusije tukanzisha DECI badala ya benki; maana hata fedha zilizotolewa na makatibu wetu
 kama ziko kwenye mikono salama," alisema na kuongeza;“Jamani, nazidi kupata shaka na kutokuwa na imani na wenzetu hawa wanaoshughulika na uanzishwaji wa benki hii kwa sababu hata ile hundi ya sh. milioni 10 iliyotolewa mbele ya Mwenyekiti wetu, (Rais Jakaya Kikwete) wakati akizindua benki hii pale Ukumbi wa Chuo cha Mipango, fedha zake mpaka sasa hazijulikani zilipo, sasa kwanini nisiwe na shaka?,” alihoji Bulembo.
Bulembo alisema tayari ameshawaandikia barua makatibu hao akiwataka kusitisha kupeleka fedha benki kwa ajili ya benki hiyo mpaka hapo atakapopata ufafanuzi zaidi wa zilipo fedha zilizotolewa awali na kujiridhisha na jitihada za kuendelea na mpango huo.“Kama kuna watu waliokula fedha hizi wazirudishe haraka vinginevyo watashtakiwa bila kujali nyadhifa zao,” alisema.
Wakichangia kwa nyakati tofauti kuhusu kuanzishwa kwa benki hiyo, Wajumbe wa Baraza Kuu hilo wameeleza kusikitishwa kwao na siri nzito inayofanywa na viongozi wa jumuiya hiyo taifa kuhusu kiasi cha fedha zilizokusanywa hadi sasa.Mjumbe wa Baraza hilo, William Malecela, aliwataka wajumbe wenzake wasikubali kupoteza muda kwa ajili ya kujadili kuanzishwa kwa benki hiyo. 
“Tuna mambo mengi ya kujadili hapa tena ya msingi, hivyo tusikubali kujadili benki ambayo ni kiinimacho. Hakuna benki hapa bali tunapoteza muda wetu bure.“Hawa waliyoleta wazo la kuanzisha benki hii hawafai na kwa sheria za nchi kama vile ya China, hawa wangehukumiwa kunyongwa au kupigwa risasi kwa sababu wametudanganya kwani walikuja katika jumuiya hii au kwa vile waliikuta ikiwa imekufa,” alisema Malecela.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa jumuiya hiyo mkoani Mbeya, Fatuma Kasenga, alishauri hatua za haraka zichukuliwe ili kujua ukweli wa kuanzishwa kwa benki hiyo.Alisema ni jambo la kutia aibu kuona benki iliyozinduliwa na Mwenyekiti wa CCM, kwa ajili kuinua uchumi wa jumuia yake kuwa ya kisanii zaidi.
“Tusikubali kukidhalilisha Chama chetu wala rais wetu. Leo ndiyo nimejua kwamba siasa ni uongo. Viongozi wetu wa jumuiya wanajigamba kwamba kuna benki kumbe si lolote wala si chohote,” alisema.
Benki hiyo iliyozinduliwa na Rais Kikwete iliingiwa ubia baina ya Kampuni mmoja (jina tunalo) na Jumuiya ya Wazazi.

No comments:

Post a Comment