07 August 2013

MJUMBE CCM KIZIMBANI KWA KUDAIWA KUBAKA


Na Israel Mwaisaka, Kyela
MJUMBE wa Kamati ya Siasa ya Chama Cha Ma p i n d u z i ( C CM) wilayani Kyela, Mkoa wa Mbeya, Joseph Mwaipopo (65) ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Fubu, Kata ya Ikama amefikishwa jana katika Mahakama ya Wilaya Kyela akituhumiwa kumbaka na kumsababishia maumivu makali mtoto wa dada yake, mwenye umri wa miaka 21
.Mwendesha mashitaka wa Jeshi la Polisi wilayani Kyela Nicholaus Tiba aliiambia mahakama hiyo kuwa Julai 16, mwaka huu saa 4 asubuhi mtuhumiwa alimbaka mtoto wa dada yake walipokuwa kwenye shamba la matikiti ambako walikuwa wanamwagilia maji katika shamba hilo.
Alidai mlalamikaji baada ya kufanyiwa kitendo hicho alitoa taarifa katika ofisi ya Serikali ya kijiji cha Fubu na baada ya hapo walitoa taarifa katika Kituo Kidogo cha Polisi Ipinda ambao nao walimpeleka binti huyo katika Kituo cha afya cha Ipinda kwa uchunguzi zaidi.
Mwendesha mashtaka huyo alimweleza Hakimu Mkuu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo ya Wilaya, Joseph Luambano, kuwa mtuhumiwa huyo amefikishwa mbele ya mahakama hiyo chini ya kifungu cha 130 kifungu kidogo cha kwanza na cha pili ( b) na kifungu cha 131 (1) katika sheria ya mwenendo ya makosa ya jinai sura ya 16 ya kanuni ya adhabu iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Mtuhumiwa amekana shtaka lake na yupo nje kwa dhamana ya sh.milioni 4 na wadhamini wawili ambapo kila mmoja dhamana yake ni sh. milioni 2 na kesi hiyo imeahirishwa hadi hapo itakapotajwa tena Septemba 4, mwaka huu.
Akizungumza nje ya mahakama hiyo Mwenyekiti CCM, Dkt. Hunter Mwakifuna alisema kuwa tukio hilo limewahuzunisha wao kama chama na kuwa kwa vile limefika mbele ya mahakama wanakiachia chombo hicho kifanye kazi yake.

No comments:

Post a Comment