12 August 2013

MILIONI 40/- ZATENGWA KUWAONDOA WAFUGAJI



 Na LIlian Justice, Morogoro
BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro limetenga kiasi cha sh. milioni 40 kwa ajili ya kufanya operesheni ya kuwaondoa wafugaji walioingia kinyume cha sheria wilayani humo. Akizungumza kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Kibena Kingo alisema kutengwa kwa fedha hizo za kuendesha operesheni ya kuwaondoa wafugaji na kuhakiki mifugo iliyopo wilayani humo kutasaidia kudhibiti tatizo la ongezeko kubwa la mifugo inayoingia visivyo halali.

Alisema ni vyema operesheni hiyo ikafanyika wakati wa kiangazi kabla ya shughuli za kilimo kuanza kwani ongezeko la mifugo husababisha migogoro inayopelekea ugomvi na hatimaye wananchi kupoteza maisha. Aliwasisitizia madiwani na viongozi wa ngazi mbalimbali kushirikiana katika zoezi hilo ili kufanyika operesheni hiyo wakati itakapoanza na kuacha kutetea watu watakaobainika wameingia bila utaratibu kwani wenye mamlaka ya kusema ni wananchi wenyewe wa vijiji husika na si wao.
Pia aliwaagiza watendaji katika halmashauri hiyo kuanzia ngazi ya vijiji kushirikiana katika kufanikisha zoezi la ujenzi wa madarasa ili wanafunzi watakapochaguliwa kusiwe na tatizo la uhaba wa madarasa. "Pamoja na kusimamia suala la ujenzi wa madarasa lakini pia msimamie suala la uboreshaji wa elimu ya msingi na sekondari kwani kumekuwa na tatizo la baadhi ya wanafunzi kuchaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari lakini hawajui kusoma na kuandika," alisema.
"Suala la uboreshaji wa elimu ya sekondari liende sambamba na uboreshaji wa elimu ya msingi kwani kwenye shule ya msingi hakuna madarasa, nyumba za walimu matundu ya vyoo kwa wanafunzi," aliongeza kusema. Naye Diwani wa Kata ya Lundi, Ally Mkata alisema katika shule ya sekondari Lundi kuna matumizi mabaya ya fedha kwa mwalimu mkuu huyo kutokana na shilingi milioni kumi na tatu kutumika kinyume na taratibu.
Akijibu tuhuma hizo Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Charles Madiga alisema kuwa, suala hilo linafanyiwa kazi na kwamba mwalimu mkuu wa shule hiyo ataanza kukatwa fedha hizo kwenye mashahara wake wa mwezi Agosti. Naye Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Kingo aliagiza pamoja na mkuu wa shule hiyo kukatwa mshahara wake lakini ni vyema pia akaelezwa kuwa alichokifanya ni kosa kinyume na utumishi wa umma na kwamba hatua nyingine zichukuliwe dhidi yake.
Naye Diwani wa Kata ya Kiroka, Robert Serasera alisisitizia watumishi wa halmashauri kusaidia suala la upimaji wa maeneo kwa wananchi kwenye vijiji vya halmashauri hiyo ili kuepusha usumbufu unaotokea kutokana na maeneo yao kutopimwa kisheria

No comments:

Post a Comment