Na
Mwandishi Wetu, Njombe
MAMLAKA ya
Mkoa wa Njombe kwa kushirikiana na Program ya Tunajali zimechangisha zaidi ya
sh.milioni 10 kuwawezesha watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu
mkoani humu kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
CHF hufanya kazi kiwilaya
kugharamia huduma za afya kwa watu walio kwenye sekta isiyo rasmi kwenye maeneo
ya vijijini. Katika mpango huo mwananchi anatakiwa kulipa kiwango fulani cha
fedha wakati wa usajili kisha pamoja na kaya yake hupata huduma bora za afya
kwa mwaka mzima.
Uchangiaji watoto hao
ulikuwa ni sehemu ya uzinduzi wa kampeni iitwayo “Jali Afya Yako, Jiunge na CHF
Leo” inayofanywa na Program ya VVU na UKIMWI ya Tunajali inayofadhiliwa kwa msaada
wa Watu wa Marekani kupitia Shirika la Misaada ya Kimataifa (USAID) kama sehemu
ya Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kupambana na UKIMWI (PEPFAR).
Katika shughuli hiyo
iliongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Aseri Msangi, ambapo kati ya fedha hizo
ahadi ilikuwa ni sh. 8,037,000 na fedha taslimu zilikuwa sh. 2,138,000.
Fedha zilizopatikana katika
hafla hiyo zinatosha kuwaunganisha watoto 5,087 na CHF kwani kundi la watoto
watano linagharimu sh. 10,000 kujiunga na Mfuko huo.
Akizindua kampeni hiyo
inayolenga kuhamasisha watu kujiunga na CHF, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, alisema
watu wengi bado hawajajiunga na mfuko huo na matokeo yake ni hukosa huduma za
afya wanapozihitaji kwani hushindwa kulipa sh. 2,000 ya papo kwa papo ya
usajili wanayotakiwa kulipa watu wasio na bima ya afya kila wanapoumwa.
Mkurugenzi Uendeshaji wa
Tunajali, Dkt. Joseph Ng’weshemi, alisema kuwa changamoto za upatikanaji wa
huduma za afya za kutosha na endelevu bado ni kubwa nchini na hilo ndilo
lililoisukuma Programu yake kubuni.
Dkt. Ng’weshemi alisema
kuwa umaskini na kutokuwa na kipato cha uhakika vimewafanya wananchi wa kawaida
kuwa na wakati mgumu kuchangia mahitaji yao binafsi ya huduma za afya.
Serikali nayo kwa upande
wake imekuwa ikijaribu kugawa rasilimali zake kwenye vipaumbele vyake kikiwemo
cha afya ambapo inategemea sana wahisani.
Kampeni hiyo itakayofanyika
katika wilaya zote za Mkoa wa Njombe, itaielimisha jamii kuhusu dhana ya bima
ya huduma za afya na wajibu wa wananchi katika kuwekeza katika afya zao.
Pia itahamasisha wanajamii na hasa wale wanaoishi na VVU kujiunga na CHF
hasa ikizingatiwa kuwa maambukizi ya VVU mkoani hapa ni makubwa zaidi nchini
ambapo ni asilimia 14.8.
No comments:
Post a Comment