01 August 2013

MAHAKAMA YAITUPA RUFAA YA NSAZUGWAKO



MAHAKAMA ya Rufaa Dar es Salaam imetupilia mbali rufaa iliyokatwa na aliyekuwa Mgombea Ubunge wa Jimbo la Kasulu Vijijini kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Nsanzugwako, aliyekuwa akipinga uamuzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora uliotolewa Mei 3,2012, anaripoti Rehema Mohamed.

Nsanzugwako alifungua kesi ya uchaguzi katika Mahakama Kuu ya Tabora kupinga matokeo ya ubunge wa Jimbo hilo mwaka 2010 yaliyompa ushindi, Agripina Buyogera, kupitia Chama Cha NCCR Mageuzi baada ya kutoridhishwa na matokeo ya uchaguzi huo.
Katika kesi hiyo Mahakama Kuu Kanda ya Tabora ilimpa ushindi Bugogera.
Uamuzi wa kutupa rufaa hiyo ulitolewa katika Mahakama ya Rufaa jana na jopo la majaji watatu waliokuwa wakiisikiliza ambao ni Jaji Nathali Kimaro, akisaidiana na Jaji Salum Massati na Jaji William Mandia.
Katika uamuzi huo wa kutupa rufaa hiyo, majaji hao walisema kuwa baada ya kuangalia mwenendo mzima wa shauri hilo wameona kuwa Jaji Haruna Songoro wa Mahakama Kuu ya Tabora alitimiza wajibu wake kikamilifu kwa kuchambua ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo wakati kesi hiyo ilipokuwa ikisikilizwa na hawakubaliani na maelezo ya Nsanzugwako kuwa mahakama hiyo haikuchambua ushahidi huo kama ilivyotakiwa.
Walisema kuwa, katika hoja ya kwamba Nsanzugwako alitolewa maneno ya kashfa katika mikutano ya kampeni ya Bugogera walisema kuwa, Jaji Songoro alikuwa sahihi kutilia mashaka kama mlalamikiwa alikashifu.
Ilielezwa kuwa, kwa mujibu wa sheria ya maadili ya uchaguzi ambayo vyama vyote vilisaini inapotokea mgombea ametolewa lugha ya kashfa au matusi anatakiwa kwenda Tume ya Uchaguzi kutoa malalamiko ambapo kwa upande wa Nsanzugwako hakufanya na hivyo kufanya malalamiko yake kutokuwa na nguvu.
Kutokana na sababu hizo,majaji hao wametupilia mbali rufaa hiyo kwa gharama.
Katika rufaa yake Nsanzugwako malalamiko makubwa ni kwamba Buyogera wakati wa mikutano yake ya kampeni, alimtolea maneno ya kashfa akimtuhumu mchawi na alishiriki kumuua aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, Tadi Magayane.
Pia alidai kuwa, Buyogera alimtuhumu kuwa ni mkorofi, alikuwa anashiriki uchaguzi kupitia ‘chama cha wala rushwa na mwizi kwa sababu alifuja fedha za jimbo hilo sh. milioni 31.”

No comments:

Post a Comment