19 August 2013

KIBADENI:SIMBA ITAANZA KAMA MAN UNITED



Na Shaban Mbegu
KOCHA mkuu wa timu ya Simba Abdallah Kibaden amesema kuwa hana hofu na kikosi chake, japokuwa amekiri kuwa kitakuwa na changamoto nyingi.Simba msimu huu ilitema baadhi ya wachezaji wengi waliokuwa katika timu hiyo msimu uliopita kutokana na sababu mbalimbali na kutengeneza kikosi kipya huku wakiwapa zaidi nafasi vijana.

Baadhi ya wachezaji waliotemwa ni Haruna Moshi, Juma Nyoso, Juma Kaseja, Amiri Maftah, Abdallah Juma, Mussa Mude, Salum Kinje Komabil Keitha, Paul Ngelema na Felix Sunzu.Kibadeni aliyezaliwa Oktoba 11, 1949, Mbagala Kiburugwa, Dar es Salaam alisema anaamini kikosi chake kitaanza vizuri ligi hiyo japokuwa kimeundwa kipya. 
Kibadeni ambaye anadai alitungwa jina hilo mwaka 1959 na watoto wenzake kutokana na kucheza soka ya nguvu akiwa mdogo na mfupi, ambalo limefunika jina lake halisi la Abdallah Athumani Seif alisema Simba itafanya maajabu ambayo hayakutarajiwa.
"Nina kikosi imara ambacho ni cha ushindani kilichochanganyika vijana na wakubwa, naamini mchanganyiko utakuwa na faida kubwa msimu huu," alisema.Kibadeni aliyejiunga na Simba Februari 2, 1969 ikiitwa Sunderland, akitokea Kahe Republic ya Mtaa wa Kongo na Mchikichi, Kariakoo alisema wamefanya maandalizi ya kutosha na atatoa salamu katika mchezo wa kwanza dhidi ya Rhino.
Kocha huyo aliyengoza Simba mwaka 1974 kuwa klabu ya kwanza na pekee Tanzania kufika nusu fainali ya Klabu Bingwa Afrika hadi sasa alisema kama ilivyofanya Manchester, Simba ndiyo itafanya hivyo.
"Tumeondoka mapema ili tukazoee mazingira, naamini tutafanya kama ilivyokuwa kwa Man United ambayo ina kocha mpya kama ilivyo Simba," alisema.
Kocha huyo aliongeza kuwa uwepo wa wachezaji wapya kama Andrew Ntala, Adeyoum Saleh, Issa Rashid na Betram Mombek, anaamini watakuwa chachu ya kufanya vizuri msimu huu.
Pia Kibadeni aliyeifunga mabao matatu peke yake mwaka 1977 katika ushindi wa 6-0 dhidi ya Yanga, alisema wachezaji wake wawili waliobaki wakifika timu itazidi kuimarika.
"Bado Tambwe (Hamis) na Kaze (Gilbert)hawajaripoti katika kikosi changu, viongozi wamenihakikishia watajiunga na timu hivi karibuni, naamini wakifika Simba itakuwa imetimia," alisema.
Kocha huyo ambaye mwaka 1993 aliiwezesha Simba SC kufika fainali ya Kombe la CAF akiwa kocha, rekodi ambayo haijavunjwa hadi leo ikiwa ni miaka 20, aliendelea kusisitiza kuwa mashabiki wa timu hiyo wala wasiwe na hofu na kikosi chao msimu huu.
Simba ambayo msimu uliopita ilitema ubingwa ambao ulichukuliwa na watani zao itaanza safari ya kusaka kurejesha heshima mtaa wa Msimbazi ugenini dhidi ya Rhino ya Tabora ambayo imepanda msimu huu.

No comments:

Post a Comment