29 August 2013

GRAND MALT YAMWAGA VIFAA LIGI KUU ZANZIBAR



 Na Mwajuma Juma, Zanzibar
KINYWAJI kisicho na kilevi cha Grand Malt, ambao ni wadhamini wa Ligi Kuu ya Zanzibar maarufu kama 'Grand Malt Premier League' jana wamekabidhi vifaa kwa timu 12 zinazoshiriki ligi hiyo katika hafla iliyofanyika Hoteli ya Bwawani, mjini hapa.

Mbali na kumwaga vifaa hivyo, Grand Malt pia wameongeza udhamini wao kwa waamuzi na uendeshaji wa ligi, ambapo msimu huu watatoa kiasi cha Sh milioni 200 kutoka sh. milioni 140 za msimu uliopita.Hafla hiyo maalumu ya kukabidhi vifaa na kutangaza kiasi hicho kipya cha uendeshaji wa ligi, ilihudhuriwa na viongozi na wanamichezo mbalimbali wakiongozwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Saidi Ali Mbarouk.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mbarouk alisema wamefurahishwa mno na Grand Malt kwa kuongeza udhamini wao pamoja na kutoa vifaa bora vya michezo kwa timu zote zishiriki."Tuna uhakika sasa soka ndani ya Zanzibar itazidi kusonga mbele, ombi lenu kwenu ZFA (Chama cha Soka Zanzibar), pamoja na wadau wote kutumia fursa hii kuhakikisha tunafika kule tunakokutaka.
"Nawasifu zaidi Grand Malt kwa kuendelea kudhamini Ligi Kuu ya Zanzibar na hii inadhihirisha tuko nao pamoja kwa mambo mengi, nasi pia tunapaswa kuwaunga mkono kwa kutumia kinywaji chao," alisema.Naye Mkurugenzi wa Masoko wa Grand Malt, Kushillah Thomas alisema, kinywaji hicho kitaendelea kushirikiana na watu wa Zanzibar katika kuhakikisha wanafanikiwa kwenye malengo yao.
"Udhamini huu ni mwanzo tu na tunaamini utasaidia kwa kiwango kikubwa kufanikisha malengo ya soka ya Zanzibar," alisema.Viongozi wa ZFA nao walikiri kufurahishwa na udhamini huo na kusema, wanaamini Ligi Kuu ya Grand Malt msimu huu itakuwa na ushindani mkubwa zaidi.
KMKM ndio waliofanikiwa kutwaa ubingwa huo msimu uliopita, wakiwa ni mabingwa wa kwanza toka kuanza kwa udhamini wa Grand Malt.
Mbali na KMKM timu nyingine zinazoshiriki ligi hiyo ni Fuoni, Chuoni, Polisi, Malindi (Bandari), Zimamoto, Mafunzo, Jamhuri, Chipukizi, Kizimbani, Mtende na Miembeni.

No comments:

Post a Comment