05 August 2013

CLINTON ATAKA WATANZANIA KUJIVUNIA SERIKALI YAO


 Na Mwandishi Maalun
RAIS Mstaafu wa 42 wa Marekani, Bill Clinton, amesema Watanzania wana kila sababu ya kujivua ukweli kuwa wana Serikali ambayo inaongoza kwa kila ubunifu wa kuboresha kila lililo jema kwa ajili ya wananchi kwa nia ya kujaribu kubadilisha maisha yao kuwa bora zaidi.Aidha, Rais Clinton amesema kuwa kama taasisi yake ya Clinton Fondation kupitia Mradi wake wa Maendeleo wa Clinton Development Initiative (CDI) itashindwa kuhakikisha kuwa mradi wake wa kilimo ambao inauanzisha nchini unakuwa endelevu, basi Clinton Foundation yenyewe itakuwa imeshindwa.
Rais Clinton aliyasema hayo juzi, Ikulu, Dar es Salaa
m, wakati alipozungumza kwenye sherehe ya kutiwa saini kwa makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na Taasisi ya Clinton Foundation, ambako taasisi hiyo itasaidia maendeleo ya kilimo na wakulima wadogo wadogo kwa kuboresha kilimo chao, kiwango chao cha mazao, ubora wa mazao yenyewe na hivyo kuinua kipato chao.
Mara baada ya Rais Clinton na mwenyeji wake Rais Jakaya Kikwete, kuwa wameshuhudia kutiwa saini kwa makubaliano hayo, Rais Clinton aliwaambia waliohudhuria hafla hiyo wakulima 10 kutoka mkoa wa Iringa na waandishi wa habari kuwa;
"Makubaliano haya ni mfano mwingine wa jitihada za Serikali ya Tanzania kuboresha maisha ya watu wake. Kwa hakika, watu wa nchi hii lazima watembee kifua wazi na wanayo kila sababu ya kujivunia ukweli kuwa Serikali yao inaongoza katika kila ubunifu wa kuboresha kila lililo jema kwa ajili ya wananchi kwa nia ya kuboresha maisha yao."
Mapema marais hao wawili walikutana na kuzungumza na wakulima wadogo wadogo 10 kutoka Mkoa wa Iringa, ambako CDI imeanza shughuli zake katika kilimo na ambako makubaliano yaliyotiwa saini juzi yataelekeza nguvu zake.
Alisema chini ya mradi huo litaanzishwa shamba la mfano kwa ajili ya wakulima kuona mbinu mpya na bora za kilimo, kutoa mafunzo na kushiriki uzalishaji.
Alisema kuwa mashamba ya namna hiyo yamefanikiwa sana katika nchi nyingine za Afrika ambako CDI inaendesha shughuli zake ikiwamo Malawi.
"Katika Malawi tulianza na shamba moja na sasa kuna mashamba ya mfano 21 ambayo yamekuza kipato cha wakulima mara tano na kuongeza uzalishaji mara mbili unusu,"alisema.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Rais Kikwete ameisifu Taasisi ya Clinton Foundation kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Tanzania katika miaka 10 ambayo taasisi hiyo imekuwepo Tanzania na hasa katika nyanja za afya na sasa kilimo.

No comments:

Post a Comment