30 August 2013

BRANDTS AMTUPIA LAWAMA MWAMUZI

  • UONGOZI 'WAANGUA KILIO' TFF


 Na Elizabeth Mayemba
KOCHA Mkuu wa Yanga, Ernest Brandts amemtupia lawama mwamuzi wa mechi Ligi Kuu kati ya timu yake na Coastal Union juzi, Martin Saanya kwa kushindwa kumudu mchezo huo na kutoa maamuzi yenye utata.

Katika mchezo huo uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.Akizungumza Dar es Salaam juzi mara baada ya mchezo huo kumalizika, Brandts alisema ameshangazwa na maamuzi ya mwamuzi huyo, mbaya zaidi akawapa penalti wapinzani wao iliyojaa utata, kwa madai hakuna mchezaji wake aliyeunawa mpira eneo la hatari.
"Mwamuzi amechangia kutunyima pointi tatu katika mchezo ule, maamuzi yake yalijaa utata mtupu sasa ile penalti aliyowapa Coastal, hata haijulikani ni kwa sababu gani kwa kuwa hakuna mchezaji wangu ambaye aliunawa mpira," alisema Brandts.Alisema pia ilishangaza watu wengi baada ya mchezaji wake, Simon Msuva kupewa kadi nyekundu na wakati alifanyiwa madhambi na Abdi Banda wa Coastal, lakini akampa kadi mchezaji ambaye hakuhusika na ugomvi Chrispine Odula.
Brandts alisema wanasubiri ripoti ya Kamisaa wa mchezo huo itakapotoka kama kweli alikuwa makini atabaini madudu ya mwamuzi huyo, ambaye tangu kuanza kwa mchezo alionekana kushindwa kuumudu mpambano huo.Alisema hali hii ikiendelea kwa waamuzi kushindwa kumudu michezo inayoendelea, bingwa atashindwa kupatikana kwa njia halali na badala yake, atapatikana kwa kubebwa na waamuzi.
Hata hivyo mara baada ya mchezo huo vurugu kubwa ziliibuka kwa mashabiki wa Yanga, ambao walikuwa wakitaka kumpiga mwamuzi huyo kutokana na maamuzi yake.Lakini askari ilibidi watumie maji ya kuwasha, ili kuwatawanya mashabiki hao ambao hata hivyo walikwenda kumsubiria nje.
Katika hatua nyingine, uongozi wa klabu hiyo umepeleka barua Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), wakitaka kadi nyekundu aliyooneshwa mchezaji Simon Msuva ifutwe na mwamuzi Saanya aadhibiwe.
 

No comments:

Post a Comment