31 July 2013

WANAORUHUSU WATOTO KUMBI ZA STAREHE WABANWE



 Na Mwandishi Wetu, Tanga 
  SERIKALI imeshauriwa kuwachukulia hatua kali wamiliki wa kumbi za starehe wanaowaruhusu watoto wenye umri chini ya miaka 18 kuingia katika maeneo hayo kwani kufanya hivyo ni kuvunja sheria na ukiukwaji wa haki za mtoto.
 Akizungumza na waandishi wa habari jijini Tanga jana, Mwanasheria wa Chama cha Wanasheria Wanawake (TAWLA) mkoani Tanga, Yona Lucas kila mmoja anatakiwa kutekeleza sheria hiyo na kwamba kitendo cha kumruhusu mtoto kuingia katika kumbi za starehe ni ukiukwaji wa haki ya mtoto ya kupata malezi bora. 
  Lucas alisema katika siku za hivi karibuni imeonekana ni kitu cha kawaida kuona watoto wadogo wanaingia katika kumbi za starehe huku wakifanyiwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia bila wao kujijua na wamiliki wa maeneo hayo wakifurahia kupata fedha kutokana na uwepo wa watu hao. 
   Alisema wanaohusika kufanya makosa hayo wanapaswa kuchukuliwa hatua kali kwani kwa kuwaachia ni sawa na kuwanyima haki watoto ambao wanatakiwa kukua katika misingi ya maadili. Hata hivyo, alisema  Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 inakataza mtoto chini ya miaka 18 kufanyiwa vitendo vitakavovunja haki zako, huku sheria ya ndoa ya mwaka 1971 inaruhusu mtoto wa kike kuolewa kwa idhini ya mzazi akiwa na miaka 14 na kwamba kunaonekana kukinzana kwa sheria hizo.
 Aliwataka Watanzania kupitia mabaraza ya katiba kutoa hoja zitakazopelekea katiba kutoa suluhu katika mgongano wa sheria za mtoto ,kwa kufanya hivyo kunaweza kumsaidia mtoto kukua bila kugudhiwa na vitendo vya ukiukwaji wa sheria.

No comments:

Post a Comment