05 July 2013

WAKAGUZI WAKUMBUSHWA KUZINGATIA WAJIBU


 Na Jovin Mihambi, Mwanza
WAKAGUZI wa Ndani wa Serikali wametakiwa kuandaa taarifa zao kwa wakati na kuzipeleka kwenye taasisi husika hali ambayo itasaidia kupunguza hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambazo zimekuwa zikijitokeza mara kwa mara katika baadhi ya kumbukumbu za hesabu katika ofisi za Serikali.
Hayo yalielezwa na Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Chotto Sendo wakati wa ufunguzi wa semina ya wastahiki meya, wenyeviti wa kamati za ukaguzi na wakaguzi wa ndani wa halmashauri za majiji, manispaa, wilaya na miji, kanda ya ziwa iliyofanyika jijini humo.

Alisema kuwa uandaaji wa taarifa mapema na kuziwasilisha kwa wakati katika ngazi zinazohusika pia ni kuwajengea uwezo wakaguzi wa ndani na wadau wa ukaguzi wa ndani kwa kuimarisha miundombinu ya ukaguzi na kupunguza hati zenye mashaka na baadaye kupata ofisi zote za Serikali nchini kuweza kupata hati safi.
Naye mratibu wa semina hiyo, Enock Mayage alisema kuwa katika mafunzo hayo, washiriki wapatao 100 kutoka Mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu, watapata fursa ya kujadili kwa uwazi changamoto zinazowakabili katika ukaguzi wa ndani katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na kuzitafutia mikakati ya muda mfupi na mrefu ya kuondokana nazo kwa kutumia rasilimali zilizopo.
Aidha, alisema semina kama hiyo ilishafanyika katika Kanda ya Nyanda za Juu (Mbeya) Kanda ya Kati (Dodoma) na Kaskazini (Arusha) na kujumuisha washiriki 243 na kuongeza hadi mwisho wa semina hiyo itakuwa imehusisha washiriki 343 na kuongeza kuwa semina nyingine itafanyika katika Kanda ya Mashariki (Dar es Salaam)

No comments:

Post a Comment