05 July 2013

AVAMIWA, AUWAWA KWA RISASI


 Na Moses Mabula, Tabora
WATU watano wanaodhaniwa kuwa majambazi wamemuua mfanyabiashara mmoja kwa kumpiga risasi tumboni katika Kijiji cha Nsungwa wilayani Kaliua mkoani Tabora.
Tukio hilo limetokea hivi karibuni ambapo majambazi hao wenye silaha za kivita waliteka kijiji hicho kisha kupora mali mbalimbali katika maduka ya wafanyabiashara wa kijiji hicho cha Nsungwa.

Kamanda wa Polisi mkoani Tabora, Peter Ouma alisema kwamba majambazi hao walimuua January Robert na kuiba vitu mbalimbali vya dukani pamoja na fedha taslimu shilingi 370,000 kisha kutoroka.
Alisema kuwa marehemu Robert aliuawa wakati akijaribu kutoa msaada wa kuzuia wizi huo usifanyike katika maduka hayo ndipo watu hao wakamfyatulia risasi tumboni na kufariki dunia papo hapo.
Kamanda Ouma alisema mara baada ya tukio hilo polisi ilifanya msako mkali na kufanikiwa kumpata mtuhumiwa mmoja Bahati Masanja ambaye inadaiwa kuwa ni miongoni mwa waliofanya mauaji ya mfanyabiashara huyo.
Alisema kwamba watu hao wanaodaiwa kuwa watano walivamia Kijiji hicho na kuvunja vibanda vitatu vya biashara na kuiba vitenge, vitambaa, vocha zenye thamani ya shilingi 40,000 na fedha taslimu kiasi hicho na kisha kukimbilia kusikojulikana.
Hata hivyo aliwataka wananchi Mkoa wa Tabora kushirikiana na jeshi hilo kwa kutoa ushirikiano ili kuweza kufanikiwa kukamatwa kwa watu hao kwani "watu hao tunaishi nao ni majirani zetu."alisema.

No comments:

Post a Comment