31 July 2013

WAGONJWA WATB,UKOMA KUNUFAIKA NA MATIBABU



 Na Grace Ndossa
SHIRIKA lisilokuwa la kiserikali la Ujerumani (GLRA), limekabidhi magari mawili na pikipiki 10 kwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kusaidia waratibu wa kifua kikuu na ukoma waweze kuwafikia walengwa sehemu walipo kwa muda mwafaka.

Akikabidhi magari hayo mwakilishi wa shirika hilo GLRA kwa upande wa Tanzania Burchard Rwamtonga alisema kuwa magari hayo pamoja na pikipiki yana thamani ya sh. milioni 124 kwa ajili ya kitengo cha kudhibiti kifua kikuu na ukoma kilicho chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ili kupata huduma kwa wakati.
Pia alisema kuwa shirika hilo linakabiliwa na changamoto ya ucheleweshaji wa upatikanaji wa msamaha wa kodi na VAT kwa magari, pikipiki na vipuri vinavyoingizwa nchini kwa ajili ya matumizi ya mpango wa kudhibiti kifua kikuu na ukoma.
Alisema kuwa magari pamoja na pikipiki zilizotolewa ziliingizwa nchini Desemba 2011, shirika lilipata kibali cha msamaha wa kodi na kutoa magari na pikipiki Desemba mwaka 2012, hivyo vifaa hivyo vilikaa bandarini kwa muda wa mwaka mmoja na kugharimu shirika sh. milioni 13 kama gharama za matunzo.
Naye Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Seif Rashidi alisema kuwa wametoa msaada kwa wakati mwafaka ili kubadilisha magari na pikipiki zilizochakaa.
Pia alitoa agizo kwa watumiaji wa vyombo hivyo katika mikoa yote Tanzania kuyatunza magari pamoja na pikipiki ili yaweze kuwa katika hali nzuri na hivyo kuweza kufanya kazi kwa muda mrefu zaidi

No comments:

Post a Comment