26 July 2013

VYUO VIKUU KUTAFITI TATIZO LA AJIRA



Na Grace Ndossa
BARAZA la Vyuo Vikuu la Afrika Mashariki (IUCEA), linafanya tafiti katika nchi tano za Afrika Mashariki kuangalia ubunifu na uwezo walionao wanafunzi pamoja na changamoto zilizopo katika elimu ya vyuo vikuu katika kupata ajira.

Kauli hiyo ilitolewa Dar es Salaam jana na Katibu Mtendaji wa baraza hilo, Profesa Mayunga Nkunya alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari kuhusu kongamano litakalofanyika Nairobi na kuunganisha Baraza la wafanyabiashara la Afrika Mashariki (EABC) na kujadili ni wanafunzi wenye sifa gani wanaotakiwa katika soko la ajira.
Alisema kuwa utafiti huo unafanyika kwa miezi mitatu na kuweza kujadili katika kongamano hilo ambalo litajumuisha wafanyabiashara wa Afrika Mashariki ni vipaji gani walivyokutana navyo katika elimu ya juu na ubunifu ili kueleza wafanyabiashara hao.
Alisema kuwa hii ni kutokana na vijana wengi wanamaliza shule hawana ajira wanabaki mitaani, kutokana na elimu wanayoipata hivyo, mfumo wa elimu unatakiwa uendane na kile ambacho anaenda kufanya katika eneo la kazi.
"Kongamano hilo litajadili na kufahamu wafanyabiashara wanahitaji watu wa namna gani au wanafunzi wenye sifa gani katika nafasi za ajira kwani kwa Tanzania fursa nyingi zinachukuliwa na wageni kutokana na wanafunzi wanaomaliza elimu ya vyuo vikuu hawana ujuzi unaotakiwa sokoni," alisema Profesa Nkunya.
Alisema kuwa washiriki watakuwa ni vyuo vya elimu ya juu, wafanyabiashara wa Afrika Mashariki, pamoja na washiriki mbalimbali ili kujadili ni wanafunzi wa namna gani wanaohitajika kwenye soko la ajira.
Hata hivyo alisema kuwa katika mkutano huo watajadili ni vitu gani vinatakiwa kufanyiwa maboresho na kujadili changamoto zilizopo katika elimu ya vyuo vikuu.
Profesa Nkunya alisema kuwa kwa sasa wanaangalia utaratibu ambao utakuwa unaangalia uwezo wa kila mwanafunzi ili kila mmoja aweze kwenda chuo kikuu badala ya kumpima mtu kwa kutumia mitihani.




No comments:

Post a Comment