26 July 2013

SERIKALI YAPIGA STOP UNYWAJI POMBE



Na Leah Daudi
SERIKALI imepiga marufuku unywaji wa pombe muda wa kazi wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro hali hiyo imeelezwa kuchangia utengenezaji na unywaji zaidi wa pombe za kienyeji ikiwemo gongo. Serikali wilayani humo inazuia unywaji wa pombe hadi saa 9:00 alasiri kwa pombe zote, licha ya kufanikiwa kwa operesheni hiyo lakini inaelezwa kulegalega kwenye pombe za kienyeji na kuchangia kuongezeka kwa kiasi kikubwa.

Wananchi ambao walizungumza na gazeti hili kwenye Kata za Mashati, Tarakea na Mkuu walisema kuwa askari wamekuwa wakizunguka kwenye maeneo yanayouza vileo kama bia na pombe kali pekee, huku wakishindwa kabisa kudhibiti uuzaji wa pombe za kienyeji na unywaji ukiongezeka. Mmoja wa mwananchi ambaye anafanya biashara ya vileo, Prediganda Marandu alisema kuwa askari wamekuwa wakitoza faini watu wanaokunywa pombe muda wa kazi lakini wamekuwa hawatoi risiti kwa faini wanazotoza.
"Wakija wakikuta mtu anakunywa bia wanataka shilingi 50,000 na anayekunywa anatozwa faini lakini cha kushangaza ni kwamba risiti hawatoi, lakini wananitoza faini hapa nyuma yangu kuna watengenezaji wa gongo lakini hawaendi kuwakamata," alisema. Baadhi ya wananchi ambao hawakutaka majina yao yataje hapa walisema kuwa operesheni hiyo ya kukamata watu wanaokunywa pombe muda wa kazi ni nzuri ila tatizo imegeuka mradi kwa baadhi ya Polisi na watendaji waliopewa jukumu hilo.
Mkuu wa Wilaya ya Rombo, Elinasi Pallangyo alisema kuwa malalamiko yanayoelezwa na wananchi juu ya polisi kuomba rushwa hawezi kukataa kwani baadhi ya polisi wamekuwa siyo waaminifu, hivyo kusababisha mazingira magumu katika utekelezaji wa operesheni hiyo.
Gazeti hili lilimtafuta Kamanda wa Polisi Mkoani hapa Robert Boaz kuzungumzia askari wake kulalamikiwa kuhusika na vitendo vya rushwa ambapo alisema malalamiko hayo hayajamfikia ila anataarifa za operesheni inayoendelea wilayani Rombo ya kuwakamata watu wanaokunywa pombe muda wa kazi ikiwemo pombe za kienyeji. Alisema kama wananchi wana ushahidi wa kutosha juu ya Polisi kuhusika katika rushwa basi wajitokeze ili zoezi hilo liweze kufanikiwa kabisa tofauti na ilivyo hivi sasa ambapo bado operesheni inaendelea.

No comments:

Post a Comment