26 July 2013

AJALI YAUA WAWILI, YAJERUHI WANNE



Na John Gagarini, Kibaha
WATU wawili wamefariki dunia na wengine wanne kujeruhiwa baada ya magari waliyokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso eneo la Vigwaza wilayani Bagamoyo mkoani Pwani. Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani humo, Ulrich Matei alisema kuwa watu hao walifariki papo hapo mara baada ya ajali hiyo.

Matei alisema kuwa ajali hiyo ilitokea jana eneo la Mtupila majira ya asubuhi ambapo waliofariki ni madereva wa magari hayo. Alitaja majina ya madereva hao kuwa ni Mohamed Athuman (32) aliyekuwa akiendesha gari aina ya Coaster yenye namba T 590 BJS likitoka Morogoro kwenda Dar es Salaam na Hemed Mohamed (34), aliyekuwa akiendesha gari aina ya Canter namba T 102 CXW likielekea Chalinze.
"Chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa Canter kuhama kwenye upande wake na kwenda upande mwingine na kukutana uso kwa uso na kusababisha ajali hiyo," alisema Matei. Aidha alisema kuwa majeruhi walipelekwa kituo cha afya cha Mlandizi huku maiti zikiwa zimepelekwa Hospitali ya Tumbi kwa ajili ya uchunguzi

No comments:

Post a Comment