12 July 2013

UPUNGUFU WALIMU WA SAYANSI WAITESA SERIKALI


 Na Mohammed Mhina,
wa Jeshi la Polisi
WILAYA ya Handeni m k o a n i T a n g a , inakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu wa masomo ya Sayansi katika shule zake za sekondari wilayani humo.
Ofisa Elimu shule ya Sekondari wilayani Handeni, Simon Mdaki alisema wilaya hiyo yenye jumla ya shule 31 za Sekondari zikiwemo 29 za Serikali na mbili za binafsi, ina walimu 58 tu wa masomo ya sayansi wakati ambapo mahitaji ni walimu 158 na hivyo kuwa na upungufu wa walimu 100.

Alisema kati ya walimu 125 wa sekondari waliopelekwa Handeni mwaka huu kufundisha katika shule mbalimbali wilayani humo, ni walimu saba tu wenye fani ya masomo ya sayansi jambo ambalo alisema bado ni kikwazo kwa somo hilo kupatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Mdaki alisema kuwa uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi wilayani Handeni, umechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza ufaulu wa wanafunzi kwa somo hilo katika mitihani yao ya taifa mwaka jana.
Alisema ni asilimia 30 tu ya wanafunzi wa kidato cha nne waliofanya vizuri katika somo hilo mwaka jana ambapo asilimia 70 kati yao walifeli jambo ambalo limeleta changamoto kubwa na kuifanya wilaya hiyo kujipanga upya kukabiliana na hali hiyo ili kuongeza kiwango cha ufaulu baadaye mwaka huu.
Alitaja tatizo lingine linalozikabili shule nyingi za Sekondari wilayani humo kuwa ni ukosefu wa vyumba na vifaa vya maabara kwa ajili ya wanafunzi kujifunzia mambo kwa vitendo badala ya nadharia pekee.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Muhingo Rweyemamu akizungumzia tatizo hilo alisema kuwa Serikali imepeleka maabara ya sayansi inayojongea (Mobile Laboratory) katika shule nne za sekondari zenye walimu wa Sayansi.
Rweyemamu alizitaja shule hizo zenye maabara inayojongea kuwa ni Kwamsisi, Kang'anta, Kwankonje na Ndolwa, maabara ambazo zitawawezesha pia wanafunzi wa shule jirani kusoma kwa vitendo masomo ya sayansi wakati serikali ikiendelea na hatua zingine za kumaliza tatizo hilo.
Alisema kwa kutumia mapato ya ndani ya Halmashauri, Wilaya ya Handeni imeanzisha utaratibu wa kujenga maabara ya sayansi katika shule za Sekondari Chogo iliyopo tarafa ya Mkumburu na katika sekondari ya Mazingara iliyopo tarafani humo.
Lakini pia alisema kuwa kuna fedha za Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari MMES II ambazo sasa zinatumika kujenga maabara katika shule ya Sekondari Sindeni iliyopo katika tarafa ya Sindeni na Kisaza iliyopo katika Tarafa ya Mzundu wilani humo ujenzi ambao unatarajiwa kukamilika baadaye mwaka huu

No comments:

Post a Comment