Na Mwandishi Wetu
MCHAKATO wa
kupitisha ongezeko la kodi ya sh. 1,000 kwa kila mtumiaji wa simu kwa mwezi
uliotokana na mabadiliko ya muswada wa fedha wa mwaka 2013 na kupitishwa na
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haukushirikisha Chama cha Makampuni ya
Simu za Mkononi (MOAT).
Kwa mujibu wa
taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na MOAT jana Dar es Salaam, imeeleza
kuwa chama hicho kilikutana na Kamati ya Bajeti ya Bunge ili kupata usahihi wa
maana ya huduma za mawasiliano ya simu kama ilivyoainishwa katika muswada wa
mwaka 2013.
Imesema katika
kikao hicho, mawasiliano ya simu yalitafsiriwa kuwa ni huduma yoyote
inayotolewa na kampuni ya mawasiliano ya simu kwa kutuma, kupokea mawimbi,
maneno, picha na sauti au habari ya aina yoyote kwa kutumia mfumo wa
kielektroniki wa picha au mfumo mwingine wowote.
“Sisi kama
waendeshaji wa mitandao ya simu hatukushirikishwa katika kujadili mfumo huu
mpya wa kulipa kodi ya sh.1,000 kwa kila laini.Tunaiomba serikali iliangalie
upya suala hili la ushuru huo ambapo kwa kufanya hivyo watawezesha ukuaji wa
mawasiliano ya simu nchini Tanzania,” ilisema taarifa hiyo.
Ukuaji wa mawasiliano ya simu nchini
Tanzania unaridhisha ambapo takwimu zinaonesha ukuaji huo ni asilimia 48, kiasi
ambacho ni sawa na watu takriban milioni 22 ambapo kati yao watu milioni 8
hutumia chini ya sh.1,000 kwa mwezi kwa mawasiliano ya simu.
Taarifa hiyo ya MOAT imeeleza kuwa
inatambua jitihada za serikali katika kukusanya kodi kwa ajili ya mipango ya
maendeleo kwa wananchi, Hata hivyo MOAT imebainisha kuwa kuanzishwa kwa kodi
hiyo kunakinzana na juhudi za kuwapunguzia mizigo ya kodi wananchi wenye kipato
cha chini.
Imesema kuwa ukuaji wa mawasiliano ya simu
katika muongo ujao utatoka maeneo ya vijijini, hata hivyo, taarifa hiyo imeeleza
kwamba uanzishwaji wa kodi mpya ya sh. 1, 000 kwa kila mtumiaji wa simu kila
mwezi utazuia juhudi zaidi za ukuaji wa huduma ya mawasiliano katika maeneo ya
vijijini kwa sababu watu wengi ambao ni wenye kipato cha chini hawataweza
kutumia mawasiliano ya huduma hiyo.
"Ulipaji wa kodi mpya ya sh.1,000 kwa kila
mtumiaji wa simu kwa mwezi utadhoofisha mafanikio yaliyopatikana katika sekta
ya mawasiliano ya simu hadi hivi leo, ambapo tumeshuhudia huduma hiyo imezidi
kuwa nafuu kwa ajili ya wote," imesema sehemu ya taarifa hiyo.
No comments:
Post a Comment