31 July 2013

SHEIN KUFUNGUA MAONESHO NANENANE



RAIS wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein kesho anatarajia kufungua maonesho ya wakulima Nanenane mkoani Dodoma na kufungwa na Rais Jakaya Kikwete, anaripoti Mariam Mziwanda.Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika mhandisi Christopher Chiza alisema kuwa Sikukuu ya Wakulima Nanenane mwaka huu inatarajia kufanyika tena Kitaifa mkoani Dodoma katika Viwanja vya Nzuguni, Manispaa ya Dodoma.

Alisema sherehe hizo ambazo kwa kiasi kikubwa hujikita zaidi katika kuonesha mafanikio na changamoto za sekta ya kilimo zitahusisha wadau wote kuanzia ngazi ya kijiji hadi Taifa lakini badala ya kumalizika Agosti 8, mwaka huu kama ilivyozoeleka zitahitimishwa mnamo Agosti saba kutokana na kuingiliana na sikukuu ya Idi El Fitri.
Alisema sherehe hizo zinaandaliwa na kuratibiwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika pamoja na Chama cha Wakulima Tanzania (TASO) huku washiriki wakubwa wakiwa ni wadau wa sekta ya Kilimo, mifugo, uvuvi, ushirika, wajasiriamali, wizara, taasisi za serikali, sekta binafsi na watoa huduma wengine na kaulimbiu ya Nanenane mwaka huu ni 'Zalisha Mazao ya Kilimo na Mifugo kwa Kulenga Mahitaji ya Soko'

No comments:

Post a Comment