25 July 2013

SHAHIDI AELEZA SHABA ILIPOHIFADHIWA



Na Rehema Mohamed
SHAHIDI wa 10 katika kesi ya wizi wa tani 26 za madini aina ya shaba inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani, (COREFA), Hassan Othman 'Hassanoo' na wenzake wawili, Rahim Jeta (38) ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa shaba hiyo ya wizi ilihifadhiwa katika yadi ya mshtakiwa wa pili, Dkt. Najim Msenga baada ya Hassanoo kumuomba.

Shahidi huyo ambaye alikuwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Usafirishaji wa Mizingi ya Libert Express iliyohusika kusafirisha shaba hiyo, alieleza hayo mahakamani hapo jana wakati akitoa ushahidi wake mbele ya hakimu Devotha Kisoka.Huku akiongozwa na Wakili wa Serikali Tumaini Kweka, Jeta alidai kuwa baada ya kupata taarifa za gari lao, T 821 DCL Scania lililobeba shaba hiyo kutofika bandarini walilifuatilia kupitia njia ya mtandao na kubaini lilipitia barabara ya Bagamoyo hadi eneo la Bahari Beach katika Yadi ya Najim.
Alisema walipofika katika yadi hiyo, wakiwa na polisi kutoka kituo cha Oysterbay kabla ya kufanya ukaguzi, ndipo mmoja wa mapolisi hao walipompigia simu Msenga, kumtaka afike hapo lakini hakufika kwa sababu alikuwa Tanga katika msiba.Shahidi huyo alisema kwa mujibu wa polisi hao, mshtakiwa wa tatu (Msenga) alikana kuhusika na shaba hiyo, ila anachokifahamu ni kwamba Hassanoo alimuomba ahifadhi mzigo huo katika yadi yake.
Alidai kuwa shaba hiyo ilikuwa ikisafirishwa kutoka Solowezi, Zambia kuja jijini Dar es Salaam na ilitakiwa kushushwa katika bandari kavu ya Tanzania Road Haulage (TRH).Naye shahidi wa tisa ambaye ni Ofisa Utumishi wa Kampuni ya Libert - Express, Solomon Makogo (47) alidai kuwa walipofika katika yadi ya Najim, walikuta shaba hiyo imefunikwa kwa turubai jekundu na kwamba aliipiga picha.
Mbali na Hassanoo, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni mfanyabiashara Wambura Kisiroti (32) na Dkt. Msenga (50).Inadaiwa kuwa Agosti 26, 2011 Bahari Beach washtakiwa hao waliiba tani 26 za madini ya shaba yenye thamani ya sh. milioni 400, mali ya Kampuni ya Liberty Express Tanzania Ltd yaliyokuwa yakisafirishwa kutoka Zambia kwa lori kuja Dar es Salaam. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 6, mwaka huu itakapoendelea kusikilizwa

No comments:

Post a Comment