04 July 2013

RAIS WA MISRI ALIGOMEA JESHI


 CAIRO, Misri
RAIS wa Misri, Mohammed Morsi, amesisitiza kuwa yeye ndiye kiongozi halali wa Taifa hilo ambapo maandamano kati ya wapinzani na wafuasi wake, yameendelea kusababisha vifo zaidi nchini humo.
Alisema jeshi la nchi hiyo haliwezi kutatua mgogoro wa kisiasa nchini humo na hawezi kuamrishwa na yeyote ambapo mpango wa jeshi hilo kuingilia kati, itazua hali ya sintofahamu.


Rais Morsi aliyasema hayo juzi usiku katika hotuba yake na kuwataka waandamanaji kuwa watulivu. Hadi jana watu 16 wameripotiwa kufa katika maandamano ya wafuasi wake.
Awali, jeshi la nchi hiyo lilitoa saa 48 kwa Rais Morsi awe ametatua mgogoro wa kisiasa uliopo nchini humo lakini kiongozi huyo amepinga onyo la jeshi dhidi ya utawala wake.
Wakati Rais Mosri akiendelea kukabiliwa na shinikizo hilo, maofisa zaidi wa Serikali yake wameendelea kujiuzulu nafasi zao likiwemo Baraza la Mawaziri.
Chama cha upinzani cha National Salvation Front, kilisema kinaunga mkono tamko la jeshi, lakini hakipo tayari kuona jeshi hilo likifanya mapinduzi ya kijeshi.
Jumapili iliyopita, mamilioni ya wananchi nchini humo walifanya maandamano wakimtaka Rais Morsi ajiuzulu ambapo maandamano mengine makubwa yalifanyika Jumatatu wiki hii.
Taarifa zaidi zinadai kuwa, watu wanane waliuawa baada ya waandamanaji kuvamia Makao Makuu ya Chama cha Muslim Brotherhood. Wapinzani wa Rais Morsi, wanamkosoa kwa kuweka masilahi ya chama mbele na kuwapuuza watu wasiokiunga mkono chama hicho.
Rais Morsi alichaguliwa kuwa rais wa kwanza wa Kiislamu katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Juni 30,2012 baada ya kuibuka mshindi. Uchaguzi huo ulifanyika baada ya aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Hosni Mubarak kuondolewa madarakani

No comments:

Post a Comment