03 July 2013

NGASSA AANZA RASMI KUITUMIKIA YANGA


 Na Elizabeth Mayemba
KIUNGO mshambuliaji wa timu ya Taifa Tanzania, Taifa Stars Mrisho Khalfani Ngassa ni miongoni mwa wachezaji walioanza mazoezi jana asubuhi kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola Mabibo, Dar es Salaam kwa ajili ya kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom 2013/2014 na mashindano ya kimataifa.
Ngassa ameanza mazoezi ambapo hivi karibuni Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kupitia kwa Msemaji wake Boniface Wambura alisema wanatambua kama mchezaji huyo ni wa Simba kwa kuwa Yanga haikupeleka mkataba wa mchezaji huyo ndani wa shirikisho hilo.

Pia Kocha Mkuu wa timu hiyo Ernest Brands naye jana alitua nchini na kuungana na timu yake mazoezini. Kocha huyo alikuwa kwao Uholanzi kwa ajili ya mapumziko.
Yanga ilikuwa na mapumziko ya zaidi ya wiki mbili tangu kuahirisha kushiriki mashindano ya Kombe la Kagame kufuatia serikali kuzizuia timu za Tanzania kwenda kushiriki mashindano hayo kufuatia kuwepo kwa hofu juu ya hali ya usalama katika mji wa Darfur nchini Sudan.
Mbali ya Ngassa pia mshambuliaji Shaaban Kondo aliyejiunga na Yanga kama mchezaji huru akitokea nchini Msumbiji alifanya mazoezi pamoja na wachezaji wengine wote wa klabu hiyo.
Leo Yanga wataendelea na mazoezi asubuhi kwenye uwanja wa Loyola ambapo golikipa mpya aliyesajiliwa kutokea klabu ya Azam Deogratius Munishi 'Dida' ataungana na wachezaji wengine katika mazoezi hayo ya kujiandaa na msimu mpya wa 2013/2014.
Wachezaji wengine waliofanya mazoezi jana ni Ally Mustapha 'Barthez', Juma Abdul, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, David Luhende, Nadir Haroub 'Cannavaro', Salum Telela, Didier Kavumbagu, Jerson Tegete, Abdallah Mnguli, Nizar Khalfani na Frank Domayo.
Ijumaa Yanga watasafiri kuelekea Kanda ya Ziwa kwa ajili ya kulitembeza kombe la Ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom pamoja na kucheza michezo kadhaa ya kirafiki.

No comments:

Post a Comment