05 July 2013

MORSI NA HARAKATI ZA KISIASA MISRI

Na Darlin Said
ALIYEKUWA Rais wa Misri,Dkt.Mohammed Morsi, alizaliwa Agosti,1951 katika jimbo la Shargiya lililopo katika eneo la Mto Nile, Kaskazini mwa nchi hiyo.
Jina kamili la kiongozi huyo ni Moham med Mohammed Morsi Issa Ayyat ambaye ni rais wa kwanza kuweka historia nchini humo kuchaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Juni, 2012 kwa kufuata demokrasia baada ya kuondolewa madarakani Rais Hosni Mubaraka ambaye aliiongoza nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 30.
Morsi pia aliweza kuweka historia kuwa rais wa kwanza kuongoza kwa kufuata sheria za Kiislamu chini ya chama chake cha Udugu wa Kiislamu (Muslim Brotherhood).
Kwa upande wa elimu yake, mwaka 1982 Dkt.Morsi alifanikiwa kutunukiwa Shahada ya Uzamivu (PhD) katika fani ya Uhandisi katika Chuo Kikuu cha Southern California kilichopo katika Jimbo la Carifonia nchini Marekani.

Kabla ya hapo mwaka 1978 Dkt. Morsi aliwahi kutunukiwa shahada ya Uzamili katika fani ya Uhandisi katika Chuo Kikuu cha Cairo nchini Misri kabla ya kwenda Marekani.
Awali mwaka 1975 kiongozi huyo, aliyedumu madarakani kwa mwaka mmoja, alitunukiwa shahada ya Uhandisi katika chuo hicho hicho cha mjini Cairo mji Mkuu wa Misri.
Baada ya mwaka mmoja tangu kupata PhD, Dkt. Morsi alianza kufanya kazi kama Profesa Msaidizi katika Chuo Kikuu cha North Ridge nchini Califonia, ambako alitumikia cheo hicho hadi 1985.
Baada ya kuacha kazi, Dkt. Morsi alirudi nchini kwake Misri na kufanya kazi katika Chuo Kikuu cha Zagazig kama mkuu wa kitengo cha Wahandisi kati ya 1985 hadi 2010.
Wakati yupo jimboni Carifonia, Dkt. Morsi aliweza kupata watoto wawili kati ya watano aliokuwanao ambao wana uraia wa nchi hiyo.
Mwaka 1977, Dkt. Morsi alijiunga na harakati za kisiasa kama mwanachama wa chama kinachosimamia sera za Kiislamu cha Udugu wa Kiislamu.
Mbali na hilo, Dkt. Morsi alichaguliwa kama mwanachama wa Mkutano wa Kimataifa wa Vyama vya Siasa na Taasisi na mwanachama mwanzilishi wa kamati ya mradi wa Misri wa kupinga uongozi usiofuata demokrasia (Zionism).
Mwaka 2000 mpaka 2005, Dkt. Morsi alifanikiwa kuwa mbunge binafsi katika bunge la nchi hiyo tangu chama chake kizuiliwe kuteua wagombea urais, kwa mujibu wa sera zilizowekwa na Rais wa zamani, Hosni Mubarak.
Wakati wa uongozi wa Hosni Mubarak,Dkt. Morsi alikamatwa na jeshi la nchi hiyo kutokana na kupinga serikali iliyokuwa madarakani.
Juni 24, 2012, Morsi aliweza kuweka historia nchini Misri baada ya kuwa rais wa kwanza wa kuchaguliwa kwa kufuata demokrasia.
Pia aliweza kuweka historia kuwa rais wa kwanza kuongoza kwa kufuata sheria za Kiislamu nchini chini ya chama cha Muslim Brotherhood.
Bw.Morsi ni rais wa tano kuongoza nchi hiyo ila ni wa kwanza asiyewekwa na jeshi hivyo uchaguzi wake ulitengeneza sura mpya ya nchi hiyo katika historia.
Baada ya ushindi huo, katika hotuba yake alisikika akisema kuwa yeye ni rais wa wa-Misri wote na atashirikiana nao katika kulisukuma gurudumu la nchi hiyo ili iweze kusonga mbele kiuchumi tofauti na uchumi walionao pamoja na kudumisha umoja wao.
Bw.Morsi alianza kazi kwa kasi zaidi, kwani Agosti, 2012 aliwatimua baadhi ya maofisa wa jeshi kama rais wa nchi hiyo.
Moja ya ahadi zake Bw.Morsi ni kuinua uchumi wa nchi hiyo ahadi ambayo imeonekana kushindwa kuitekeleza kwa wananchi wake na kusababisha Wamisri kuanza maandamano ya kutaka aondoke baada ya kukaa mwaka mmoja madarakani.
Hivyo kutokana na hali hiyo Bw.Morsi alionekana kukaidi maamuzi ya wananchi na kuhoji kuwa yeye ndiye rais halali wa nchi hiyo.
Kutokana na pingamizi lake likasababisha maandamano yaliyodumu kwa siku nne kumshinikiza atoke madarakani katika viwanja vya Tahrir Square katika mji mkuu wa nchi hiyo
Hivyo ili kunusuru madhara ambayo yangeweza kutokea Mkuu wa Jeshi la nchi hiyo Bw.Abdel- Fatah El-Sis walimpa masaa 48 kujiuzuru ili kuleta amani katika nchi hiyo amri ambayo alipinga na kusababisha kupinduliwa rasmi hapo juzi.
Kutokana na hali hiyo Mkuu wa Jeshi hilo amesikika akitangaza uamuzi wa jeshi kuchukua madaraka ili kuendelea kulinda amani kwa wananchi wa nchi hiyo.
Waandamanaji hao inasadikiwa kuwa wamesikika wakidai kuwa kiongozi huyo alikuwa anawawezesha watu wa chama chake na kuwasahau wananchi wengine kama rais.
Hadi leo jeshi la nchi hiyo limemteua Jaji Mkuu wa Mahakama ya Katiba Misri, Adly Mansour kuongoza kwa muda hadi pale utaratibu utakapokamilika ambaye kabla ya uteuzi huo aliteuliwa kuwa jaji wa mahakama hiyo Juni 30, mwaka huu kabla ya uteuzi huo.
Moja ya taratibu hizo ni pamoja na uandaaji wa katiba kutokana na nchi hiyo kutokuwa na katiba inayosimamia mamlaka ya nchi hiyo.
*Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa vyombo vya habari

No comments:

Post a Comment