Na Suleiman Abeid
ATHARI za
UKIMWI katika jamii ni kubwa ikiwemo kupunguza uzalishaji kwa kupoteza
nguvukazi.Zaidi ya asilimia sabini ya
wanaoambukizwa na kuugua UKIMWI ni watu wenye umri kati ya miaka 20 hadi 40
ambao ni vijana. Kundi hilo ndilo
linalotegemewa na familia na taifa kwa ujumla katika maisha, utendaji,
uzalishaji mali na hali ya baadaye ya Taifa.
Hivyo, ni lazima tuupige
vita UKIMWI kwa nguvu zetu zote. Tuanze kwa kuzuia maambukizo kwa wale karibu
asilimia 85 ya watu wazima ambao hivi sasa hawana virusi vya UKIMWI, ili
wabakie katika hali iliyo salama.VVU ni tatizo kubwa la maendeleo
linaloathiri sekta zote. Katika kipindi cha miongo miwili iliyopita umeenea
bila huruma na kuathiri watu katika nyanja zote za maisha na kuangamiza sehemu
kubwa ya watu wanaoshiriki katika uzalishaji mali hususan wanawake na wanaume
wenye umri kati ya miaka 20 hadi 49.
Maneno hayo yalitamkwa na
Rais wa awamu ya tatu hapa nchini, Bw.Benjamin Mkapa mwaka 2002 alipokua
akizindua rasmi sera ya UKIMWI nchini ambapo aliutangaza ugonjwa huo kama janga
la Taifa na kuwaomba Watanzania wa rika zote kushiriki kikamilifu katika vita
dhidi ya ugonjwa huo.Sera hiyo ya UKIMWI
inaeleza kwamba serikali kwa upande wake ina wajibu wa kusimamia na kuongoza
masuala ya fedha katika shughuli za Taifa kuhusu uambukizo wa VVU na kwamba
katika kipindi hicho ilitenga dola za Marekani milioni nane kwa ajili ya
shughuli hizo.
Hata hivyo kutokana na
serikali kutokuwa na fedha za kutosha ilielekeza wadau wengine ikiwemo idara
zake, taasisi za umma, halmashauri za majiji, manispaa, miji na wilaya na zile
za binafsi kushiriki kikamilifu katika mapambano hayo.Lengo kubwa ni kila mtu
kushiriki katika mapambano dhidi ya maambukizo ya virusi vinavyosababisha
ugonjwa hatari kwa kuwezesha kupunguza idadi ya maambukizo mapya miongoni mwa
jamii.
Kutokana na hali hiyo idara
na taasisi mbalimbali za serikali na mashirika ya kidini zimejitosa katika vita
hiyo kupitia semina na makongamano mbalimbali ikiwemo uhamasishaji wa upimaji
kwa hiari.Idara ya Uhamiaji nchini
katika kuunga mkono wito wa serikali hivi sasa imeanzisha zoezi la upimaji wa
hiari kwa watumishi wake nchi nzima sambamba na kutoa elimu kwa wateja wake
mbalimbali wanaokwenda katika ofisi zake kutaka huduma mbalimbali.
Kamishna msaidizi wa
uhamiaji nchini, Bi.Salome Kahamba anasema, katika kukabiliana na wimbi la
maambukizo mapya ya VVU miongoni mwa watumishi wa idara hiyo, wameanzisha zoezi
la upimaji wa hiari kwa watumishi wake ili kuweza kuwasaidia wale wote
watakaobainika kuambukizwa virusi hivyo.
Anasema, hilo litahusisha pia familia za watumishi
hao kwa vile pindi itakapotokea mmoja wa watu wanaoishi na mtumishi akaugua
UKIMWI kwa njia moja ama nyingine mtumishi huyo atalazimika kumshughulikia kwa
kipindi kirefu na hivyo kujikuta akishindwa kutimiza vizuri majukumu yake ya
kikazi.
“Idara yetu ya Uhamiaji mnamo mwaka 2003 tulikaa
chini na kutafakari janga hili la UKIMWI hapa nchini, tukaona hata sisi
tusipojitosa kupambana nalo linaweza kuwa na athari kubwa katika utendaji wa
idara yetu,
“Tuliamini wazi kwamba tukizembea, tutapoteza kwa
kiasi kikubwa nguvukazi ya idara kwa watumishi wetu wengi kupukutika kwa gonjwa
hili, hivyo tuliona ni vyema tuunge mkono juhudi za serikali katika kupambana
na maambukizo ya virusi vya UKIMWI kama alivyotangaza Rais mstaafu Bw. Benjamin
Mkapa,” anasema Bi. Kahamba.
Bi. Kahamba ambaye pia ndiye mratibu wa kudhibiti
maambukizo mapya katika idara hiyo ya uhamiaji anasema, ili kuhakikisha vita
dhidi ya maambukizo mapya inafanikiwa, idara iliwapeleka nchini Uganda baadhi
ya watumishi wake ili kwenda kujifunza mbinu za ushauri nasaha.
Anasema, mpaka hivi sasa tayari wana washauri
nasaha waliopata mafunzo watumishi 35 na pia waelimishaji rika 70 ambao
watasambazwa katika mikoa yote nchini kwa ajili ya kufanya kazi ya uhamasishaji
na ushauri nasaha utakaowezesha watumishi wote kupima kwa hiari ili kuelewa
afya zao.
“Janga hili tusipolivalia njuga linaweza kuathiri
kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi na ndiyo maana idara yetu mbali ya kuendesha
zoezi la upimaji wa hiari kwa watumishi wake, lakini pia tumeanza kuweka bajeti
maalumu kwa ajili ya kuwasaidia watumishi ambao watabainika kuwa wameambukizwa
VVU,
“Na huduma hii si lazima itolewe kwa mtumishi tu,
hata kama mtumishi atakuwa hajaambukizwa VVU lakini labda mkewe, mtoto au
mtumishi wa ndani anayeishi naye akiwa ameambukizwa pia huyu atapatiwa huduma
zote muhimu anazopaswa kupatiwa mtu mwenye VVU,”anasema Bi. Kahamba.
Anasema kutokana na hali hiyo wanahimiza watumishi
kuhakikisha wanapimwa pamoja na familia zao na kwamba kitendo cha mtumishi
kutowapeleka watu wanaomtegemea katika huduma ya upimaji kinaweza kuathiri
bajeti ya idara pale itokeapo mtumishi huyo kubaini ana mtu anayeugua UKIMWI.
“Tumewasisitiza watumishi wetu wahakikishe kwamba
hata watu wanaoishi nao wanapimwa ili waweze kufahamu afya zao hii ni pamoja na
watumishi wa ndani, hawa ni muhimu sana, maana ndiyo wanaobaki wakiwalelea
watoto wao majumbani.”
Anasema, mbali ya kuendesha zoezi la upimaji wa
hiari kwa watumishi pia idara imekuwa ikitoa vipeperushi na mabango yenye
maandishi yanayotahadharisha juu ya athari ya UKIMWI na jinsi ya kujikinga na
maambukizo mapya.
Kwa upande wake mmoja wa washauri nasaha katika
idara hiyo ya uhamiaji, Bw.Justus Kusiluka anasema suala la mtu kupima afya
yake kwa hivi sasa ni muhimu sana kwa vile ataweza kuishi bila hofu kila wakati
na anakuwa na uhakika wa kupanga mipango yake ya maisha vizuri.
Bw. Kusiluka anasema, wapo baadhi ya watu ambao
hawapendi kupima afya zao lakini wamekuwa wakiishi kwa hofu kubwa pale
inapotokea kuugua homa mara kwa mara na hivyo kuhisi tu kwamba wameambukizwa.
Anasema, “Ni muhimu kupima, usipopima unasababisha
mtu uishi maisha ya hofu, daima unakuwa na wasiwasi, lakini pia unashindwa
kupanga mipango yako vizuri, ni vizuri tukatumia hiari tuliyonayo katika
kupima,”
“Kama hujapima unapougua gonjwa lolote lile, tayari
unakuwa na wasiwasi, labda nimeathirika, lakini kwa wale walioathirika wataweza
kuelewa jinsi ya kuishi kwa matumaini na mtu anapata maelekezo ya mpangilio wa
lishe yake iweje, hivyo ataishi maisha marefu kama
wengine.”
No comments:
Post a Comment