23 July 2013

MAGARI MOSHI YAGOMA KUSAFIRISHA ABIRIA



 Na Heckton Chuwa, Moshi
MGOMO mkubwa wa usafirishaji unaoyahusu magari makubwa aina ya Coaster umetokea mjini Moshi Mkoa wa Kilimanjaro na kusababisha adha kubwa kwa wananchi waliokuwa wakisafiri katika Wilaya za Moshi Mjini na Wilaya ya Rombo, mkoani humo.Mbali na adha hiyo kwa abiria, vurugu kubwa zilitokea kati ya viongozi na madereva wa magari makubwa yanayofanya safari kati ya Rombo na Moshi mjini na wale wa magari madogo aina ya Noah.

Wakati mgogoro huo ukiendelea mmoja wa watu anayedaiwa kuwa ni dereva wa gari aina ya Noah alikimbilia kwenye hoteli ya jirani na kutoka na kisu na kumfuata kiongozi wa Chama cha Wenye Magari Makubwa Aina ya Coaster, Linus Kilawe kwa lengo la kumdhuru kabla ya kuzuiwa na wenzake.
Akizungumzia mgomo huo, Kilawe alisema wamiliki wa magari hayo wameamua kuuitisha kufuatia malalamiko yao kuhusiana na wenzao wanaomiliki na kuendesha biashara ya usafiri wa Noah kutokuzingatiwa na mamlaka husika.
"Hawa wenye Noah wanaenda umbali ambao hawaruhusiwi kisheria, hawana sare, wanatoza nauli bila ya kutoa tiketi kwa abiria huku wakibeba abiria wengi kuliko wale wanaoruhusiwa kisheria kwenye magari hayo. Wenye magari makubwa wakifanya makosa hayo huwa wanachukuliwa hatua za kisheria," alisema.
Kilawe aliendelea kusema kuwa, kwa wenye magari ya Noah kuruhusiwa kwenda umbali zaidi ya kilomita wanazoruhusiwa kisheria kumesababisha wenye magari makubwa kukosa abiria na kujikuta wakikusanya abiria njiani kama vile daladala wakati safari zao ni za umbali mrefu.
Alisema, hatua ya magari aina ya Noah kuruhusiwa kufanya biashara hiyo bila kulipia gharama za kisheria kama zile wanazotozwa wenye magari makubwa kunainyima serikali mapato ya kihalali huku mamlaka zenye kuhusika likiyafumbia macho mambo hayo.
Alisema, tayari wameshakutana na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Dkt. Ibrahim Msengi ambapo walipeleka mapendekezo yao yanayotaka pamoja na mambo mengine, wenye magari makubwa na wale wa Noah wakubaliwe kupakia abiria kwa zamu wakati masuala mengine yakifanyiwa kazi.

No comments:

Post a Comment