05 July 2013

KUNA UPUNGUFU WA SUKARI TANI 220,000


IMEELEZWA kuwa Tanzania inakabiliwa na upungufu wa tani 220,000 za sukari kutokana na changamoto mbalimbali zinazowakabili wakulima wa sukari ikiwa ni pamoja na wakulima kutowezeshwa katika masuala ya uzalishaji.
Hayo yamebainishwa jana na mchambuzi na mshauri wa masuala ya chakula na kilimo Afrika kutoka Benki ya Kimataifa ya Robo, Sierk Plaat wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maonyesho ya 37 ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba, kufuatia utafiti uliofanywa na benki ya NMB kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Alisema sukari inayozalishwa nchini ni tani 300,000 wakati mahitaji ni tani 520,000 ili iweze kukidhi mahitaji ya wananchi.
“Pengo hili la uzalishaji endapo wakulima watasaidia kuondokana na changamoto zinazowakabili itasaidia kuachana na biashara za kuagiza sukari nje ya nchi,”alisema Plaat.
Alisema ana imani sukari inayozalishwa nchini ni bora lakini kutokana na sababu mbalimbali zimechangia upungufu wa uzalishaji hali ambayo inachangia kutegemea zaidi sukari inayoagizwa kutoka nje.
Kwa upande wake, Calo Nyangaro ambaye alifanya utafiti wa stakabadhi ghalani alisema, katika utafiti wao wamebaini utaratibu wa stakabadhi ghalani unawasaidia sana wakulima endapo utasimamiwa vizuri na kuzingatiwa.
Alisema katika utafiti walioufanya kwa kushirikiana na wadau mbalimbali walitaka kubaini kama utaratibu wa stakabadhi ghalani unatoa tija kwa wakulima kwa upande wa wakulima wa korosho, ufuta, mpunga na mazao mengineyo.
Isack alisema katika utafiti huo walioufanya maeneo mbalimbali nchini wamebaini unatekelezeka kwa kiwango cha juu mbali ya changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo wakulima.
Naye, Meneja Mkuu Kitengo cha Kilimo NMB, Robert Pascal alisema benki ya NMB iliamua kufanya tafiti mbalimbali kwa lengo la kuisaidia jamii ya wakulima nchini na kunyanyua pato la taifa.
Alisema hadi sasa wametoa mkopo wa sh. bilioni 116 kwa wakulima na kuzifikia kaya 500 nchi nzima.

No comments:

Post a Comment