Na Mwandishi Wetu
RAIS Jakaya Kikwete,
ameagiza Wizara za Serikali zinazohusika na kodi na mawasiliano pamoja na
kampuni za simu za mikononi nchini kukutana mara moja kutafuta jinsi gani ya
kumaliza mvutano wa kodi mpya ya kadi za simu hizo za mikononi.
Rais Kikwete alitoa maelekezo hayo jana jioni wakati alipokutana
na viongozi wa Wizara ya Fedha, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia na
wawakilishi wa kampuni za simu Ikulu, Dar
es Salaam.
Rais Kikwete alisema lengo kuu la mkutano huo wa pamoja kati ya
Wizara hizo za Serikali na kampuni za simu ni kupendekeza jinsi gani ya kuziba
pengo la sh. bilioni 178 ambazo zitapotea katika Bajeti iwapo kodi hiyo kwa
kadi za kuongelea za simu za mikononi italazimika kufutwa na Serikali kupitia
marekebisho kwenye Mswada wa Fedha wa Bajeti ya Mwaka 2013/2014.
Rais Kikwete aliwaambia wawakilishi wa pande hizo mbili kuwa
huwezi tena kuifuta moja kwa moja kodi hiyo bila kutafuta njia nyingine za
kupata fedha za kujaza pengo hilo
la sh. bilioni 178 ambazo tayari Bunge limezipangia matumizi.
"Nawaombeni kaeni pamoja, wekeni bongo zenu pamoja, wekeni
akili yenu pamoja tutafute namna gani tunaweza kujaza pengo hili la sh. bilioni
178 endapo tutakubaliana kuwa kodi hii inawabebesha wananchi mzigo mzito na
kuwa pengine menejimenti ya kodi yenyewe ni ngumu," alisema Rais Kikwete.
Katika Bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/2014, Serikali
imeweka kodi ya Sh. 1,000 kwa mwezi kwa kila mtumiaji simu kwa ajili ya kufanya
mawasiliano kwa kutumia simu ya mkononi.
No comments:
Post a Comment