Na Mwajuma Juma, Zanzibar
RAIS
wa Heshima wa Chama cha Judo Zanzibar, Tsuyoshi Shimaoka amesema kuwa ujenzi wa
uwanja wa Judo kisiwani Pemba hautakuwa
mkombozi wa Judo pekee bali na michezo mingine. Shimaoka alitoa kauli hiyo juzi
mara baada ya utiaji wa saini wa ujenzi wa uwanja huo kati yake na Balozi wa
Japani, Masaki Okada katika ukumbi wa Judo Amaan mjini Zanzibar, ambapo Serikali hiyo ya Japani
imetoa sh. milioni 193 kusaidia ujenzi huo
.Alisema chama
cha Judo kilikuwa na hamu kubwa ya kuwa na uwanja kisiwani humo ili kuweza
kufanikisha ndoto zake za kuwa na viwanja vya Judo Zanzibar nzima."Ujenzi wa
Budokan kisiwani Pemba hautakuwa mkombozi wa Judo pekee bali na michezo mingine
pia kukamilika kwake kutakamilisha ndoto yetu ya kuwa na viwanja Zanzibar nzima,"
alisema. Sambamba na hilo alisema kuwa mara
baada ya kukamilika ujenzi huo changamoto itakayowakabili ni kuweka samani
mbalimbali pamoja na kuweka jozi za nguo za Judo na mambo mengine yanayohusu
mchezo huo, ambapo vitu hivyo vitagharimu sh. milioni 200.
Akizungumza
katika hafla hiyo balozi wa Japani, Masaki Okada alisema kuwa amefurahi sana kuona kwamba michezo ya kijapani imeenea Zanzibar na hivyo
kukamilika kwa ujenzi huo kutawapa fursa wanamichezo wa kisiwani humo kukuza
vipaji vyao vya michezo mbalimbali ambayo itachezwa katika uwanja huo wa ndani.
Michezo mingine itakayochezwa katika
uwanja huo ni pamoja na netiboli, mpira wa kikapu,Tenisi, mpira wa mikono na
kareti. Kwa upande wake Waziri wa Habari Utamaduni, Utalii na Michezo Said Ali
Mbarouk alisema kuwa Serikali kwa kushirikiana na Baraza la Michezo Zanzibar imekuwa
ikichukua juhudi mbalimbali za kuimarisha michezo, lakini haiwezi kuimarika
bila ya kuwepo na wafadhili.
Ujenzi
wa jengo hilo
unatarajiwa kuwa ni wa miezi saba na utakamilika Januari mwakani, huku gharama
za mradi mzima ukiwa ni sh.milioni 500 hadi kukamilika kwake.
.
No comments:
Post a Comment