15 July 2013

IMANI POTOFU HUCHANGIA VIFO VYA WAJAWAZITO


"|Changamoto kubwa ni upungufu wa watumishi. Tulionao ni chini ya asilimia 35 ya mahitaji ya watumishi hali ambayo inasababisha malalamiko."

SERIKALI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wamekuwa wakiendesha harakati mbalimbali za kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya hususan afya ya uzazi ili kupunguza vifo vya wajawazito wakati wa kujifungua ikiwa sehemu ya Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDG).
Madhumuni ya harakati hizo ni kupunguzwa kwa asilmia 75 kwa vifo vinavyotokana na uzazi ifikapo mwaka 2015.Miongoni mwa mikakati inayoendelea kutekelezwa ni kupandisha hadhi vituo vya kutoa huduma, kuhamasisha jamii juu ya afya ya uzazi, kujenga zanahati na vituo vya afya, kuongeza idadi ya watumishi wa kada ya afya pamoja na kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba.Hata hivyo, mratibu msaidizi wa afya ya uzazi na mtoto katika Wilaya ya Geita, Nafka Robson, anasema kuna changamoto kadhaa ambazo bado zinapelekea kuendelea kuwepo kwa vifo vya wajawazito ambavyo hutokea wakati wa kujifungua.

Anasema jumla ya wajawazito 28,012 walijifungua salama katika kipindi cha mwaka 2011 wilayani Geita huku 18,218 kati yao wakijifungulia kwenye vituo vya tiba, 4,960 wakijifungulia majumbani na 299 wakijifungulia njiani wakati wakipelekwa kwenye vituo vya kutoa huduma.
Mratibu msaidizi huyo wa afya ya uzazi na mtoto katika wilaya ya Geita anasema mwaka 2011, jumla ya wajawazito 48 walipoteza maisha wilayani humo wakati wa kujifungua, ambapo 32 walifariki wakiwa kwenye vituo vya kutoa tiba na wengine 16 walifariki katika maeneo mengine ya kijamii.
Anasema katika mwaka 2012, jumla ya wajawazito 24,702 walijifungua salama huku idadi ya vifo ikipungua kutoka 48 mwaka 2011 hadi vifo 34 ambavyo 30 vilitokea kwneye vituo vya tiba na vinne vilitokea kwenye maeneo ya jamii.
Katika robo ya kwanza ya mwaka huu, anasema jumla ya wajawazito 5,530 wamejifungua salama katika kipindi cha kati ya Januari hadi Machi, mwaka huu, huku jumla ya vifo 14 vikitokea, ambapo 13 vilitokea katika vituo vya huduma na kimoja katika maeneo mengine ya jamii.
Vilevile, anaeleza kuwa vifo vingi vinasababishwa na kutokwa damu nyingi, upungufu wa damu, maambukizi baada ya kujifungua, kifafa cha uzazi, kujitambua mapema kwa kondo la nyuma, Ukimwi pamoja na ugonjwa wa moyo.
Anasema vifo vya wajawazito vinaweza kupungua ikiwa wazazi watafuata maekelezo ya wataalamu ambao pamoja na mambo mengine wanawashauri kula chakula bora kama njia ya kuwawezesha kuwa wenye siha njema na hivyo kuzalisha damu ya kutosha.
Pia anasema baadhi ya imani au taarifa potofu miongoni mwa jamii huchangia katika madhara yanayoweza kuwapata wajawazito ikiwa pamoja na imani kuwa matumizi ya dawa za Follic Acid husababisha muda wa kujifungua kuzidi miezi tisa kama ilivyo kawaida. Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Geita, Dkt. Noel Makuza, anasema serikali imekuwa ikijitahidi kuboresha huduma za afya kwa wananchi, licha ya changamoto zilizopo.
Anasema malalamiko ya wananchi juu ya kuchelewa kupata huduma za afya katika vituo vya umma, yanatokana na idadi ndogo ya watumishi kwani wilaya hiyo ina upungufu wa asilimia 68 ya mahitaji ya watumishi wanaotakiwa.Dkt. Makuza anasema serikali imeongeza watumishi wapya 70 wa afya katika mkoa mpya wa Geita, ambapo hadi kufikia Juni 26, mwaka huu, ilikuwa imetumia zaidi ya sh.milioni 500 kununua dawa MSD, ambao walikuwa wakiendelea kusambaza katika zahanati na vituo vya afya vya mkoa huo.
“Kwa sasa tatizo la dawa tumefanikiwa kulidhibiti. Hospitali ya wilaya ya Geita ina hudumia zaidi ya watu milioni moja, idadi ambayo ni kubwa zaidi ukilinganisha na hospitali nyingi nchini,” anasema Dkt. Makuza.
Anasema wamenunua vitanda vipya katika hospitali ya Wilaya ya Geita pamoja na kuongeza upatikanaji wa huduma nyingine kwa wagonjwa. Kuhusu tatizo la jenereta la kuzalisha umeme wa akiba katika hospitali ya wilaya ya Geita, Dkt. Makuza anasema madai hayo hayana ukweli kwani serikali imelishughulikia tatizo hilo na kulipatia ufumbuzi baada ya kutoa jenereta mbili kwa hospitali hiyo.
Dkt. Makuza anaongelea kuhusu vifo vya wajawazito kwenye hospitali hiyo kwa kueleza kuwa kuna utaratibu wa kujadili malalamiko yanayotolewa na wagonjwa.
“Changamoto kubwa ni upungufu wa watumishi. Tulionao ni chini ya asilimia 35 ya mahitaji ya watumishi hali ambayo inasababisha malalamiko,” anasema.
Kwa kuzingatia hali hiyo Shirika lisilokuwa la kiserikali linalojishughulisha na ubora wa huduma za afya na urahisi wa jamii kufikiwa na huduma hizo, Tandabui Health Access Tanzania (THAT)/ Afya redio, uliwasilia nyumbani kwa John Kisyeri (27), mkazi wa eneo la Mbugani, kata ya Kalangalala wilayani humo.
Madhumuni ya safari hiyo ni kulenga kupunguza vifo vya wajawazito ambapo iliamua kuzitembelea baadhi ya familia zilizokumbwa na misiba na kutokana na akina mama kufariki wakati wa kujifungua.
“Ilikuwa asubuhi ya Mei 25, mwaka huu wakati najiandaa kwenda kazini, mke wangu Perus Mnanka (22) alinieleza kuwa anahisi dalili za uchungu, hivyo niende kazini kuaga ili niweze kurejea na kumpeleka katika hospitali ya wilaya ya Geita kwa ajili ya kujifungua,” anaanza kueleza jinsi kifo cha mkewe kilivyotokea na kuongeza:“Nilirudi nyumbani na kumpeleka hospitali ya Wilaya ya Geita, ilikuwa saa tatu asubuhi. Kama kawaida nilizuiliwa kuingia katika wodi ya wazazi na kuambiwa niende kutafuta chai kwa ajili ya mjamzito”.
Anasema baada ya kupeleka chai alirudi nyumbani kuandaa chakula cha mchana na baada ya kurudi hospitalini kupeleka chakula hicho, alielezwa kuwa mke wake hakuwa amejifungua na kwamba alikuwa akiendelea kupatiwa huduma.
“Hisia zangu zilinituma kuamini kwamba kuna kitu kisichokuwa cha kawaida kinaendelea kwani nilizuiwa kuingia kumwona. Hata simu yake ilikuwa ikiita bila majibu. Mama niliyemwacha wodini alinitaka niendelee kuwa mvumilivu wakati huduma kwa mke wangu ikiendelea, “Niliamua kurudi nyumbani kwa kuwa sio mbali na hospitali, ambako nilimpigia simu mama mkwe kumjulisha juu ya kilichokuwa kikiendelea na badaye kufanya maombi ili mke wangu ajifungue salama,” anasema mwalimu huyo wa Shule ya Sekondari Kivukoni.
Anaeleza kuwa ilipofika saa 11 jioni, alipigiwa simu kuhitajika kufika hospitali ambako daktari alimweleza kuwa jitihada zao za kumpatia huduma mke wake zimeshindikana na kuwa amefariki wakati akijifungua.
“Nililia kama mtoto mdogo. Mke wangu alikuwa na umri wa miaka 22. Ndio kwanza amemaliza shahada yake ya uhasibu. Tulikuwa na matarajio makubwa katika maisha yetu lakini maisha yake yamefikia kikomo. Namshukuru Mungu kwa yaliyotokea lakini najiuliza, ilikuwaje wakashindwa kuokoa hata maisha ya kichanga?” anahoji.
U j u m b e w a h u o THAT ulimtembelea mwalimu Kisyeri ikiwa takriban siku 21 tangu kufariki kwa mke wake, lakini mwalimu huyo mwenyeji wa Wilaya ya Tarime mkoani Mara, anatupa lawama kwa uongozi wa hospitali kutokana na uduni wa upatikananji wa huduma kwa wanawake wanaojifungua katika hospitali ya wilaya.
“Mimi kinachoniumiza zaidi sio kifo cha mke wangu. Najiuliza, kwanini afariki akiwa na mtoto tumboni? alihoji. Binadamu gani anaweza kuvumilia uchungu wa uzazi kuanzia saa tatu asubuhi hadi saa 11 jioni?. Nafikiri kuna uzembe katika utoaji wa huduma,” alidai mwalimu huyo.
Hali hiyo ya majonzi haimkabili mwalimu Kisyeri pekee, mwingine ni Bahati Joseph mkazi wa eneo la Uwanja, kata ya Kalangalala wilayani Geita, ambaye pia alidai kumpoteza mke wake Mei 24, mwaka huu, wakati akijifungua.Joseph ambaye mke wake, Roza Sekeli alikuwa na ujauzito wa pili, anadai kuwa alimpeleka hospitalini hapo saa nne asubuhi na kufariki saa 12 asubuhi wakati akiwa katika harakati za kujifungua.
Hata hivyo, Joseph anadai kuwa huduma duni inayosababishwa na upungufu wa watumishi ni sababu iliyochangia kifo cha mke wake pamoja na mtoto aliyekuwa tumboni na kuongeza kuwa alipofika hospitalini hapo mke wake aliongezwa maji ya uchungu ili kumsaidia kujifungua. Joseph anasema kuwa alielezwa kuwa uchunguzi wa madaktari ulibaini kuwa mtoto alifariki siku mbili kabla ya mama hajafikishwa hospitaini na kuwa maji ya kuongeza uchungu aliyopewa hayakuweza kusaidia mtoto kutoka tumboni kama ilivyokusudiwa.
“Mke wangu alikuwa akihudhuria k l i n i k i . Mim i mwenyewe nilimsindikiza mara mbili.Ni mapenzi ya mwenyezi Mungu lakini utajisikia vipi mzazi akipelekwa hospitali anakaa muda wote huo bila kujifungua halafu mtoto anafia tumboni,” anahoji Joseph ambaye anajihushughulisha na shughuli za kilimo.
Ziara hiyo pia ilifika nyumbani kwa Freeman Kishe, mkazi wa eneo la Bomani ambaye kama ilivyo kwa wenzake, anaeleza hisia zake kutokana na kifo cha mke wake ambacho kwa mtazamo wake kilichangiwa na ukosefu wa umeme wa akiba katika hospitali ya wilaya ya Geita.
“Mke wangu Justina Peter, alifariki Aprili 10,mwaka huu wakati akifanyiwa upasuaji wa kurekebisha mfumo wake wa mkojo ulioathiriwa na upasuaji uliofanyika siku 60 nyuma wakati alipofanyiwa upasuaji baada ya kushindwa kujifungua kwa njia ya kawaida,” anasema.
Anadai umeme ulikatika wakati wa upasuaji huo ukiendelea, ambapo jenereta haikuweza kuwashwa kwa wakati, hivyo walishindwa kudhibiti damu kuvuja na hivyo kupelekea kifo cha mke wake. Na huko katika kitongoji cha Bunyema, kijiji cha Bulangale kata ya Bukwimba wilaya mpya ya Nyangh’wale mkoani Geita, familia ya Nyanjige Katoto inaendelea kusikitika kufuatia kifo cha mtoto wao, Monica Hamis aliyefariki Aprili 3, mwaka huu, katika kituo cha afya cha Karumwa.
Kwa mujibu wa Nyanjige Katoto, Mtoto wake Monica ambaye alikuwa na umri wa miaka 42 na ambaye huo ulikuwa ujauzito wake wa nane, alifariki baada ya kutokwa damu nyingi.
Changamoto iliyojitokeza katika mazungumzo na familia hiyo ni pamoja na kuelezwa kuwa hakukuwa na kumbukukumbu sahihi za umri wa mimba aliyekuwa nayo marehemu kwani hakuwahi kuhudhuria kliniki katika kipindi chote cha miezi zaidi ya mitano ambacho inasadikiwa kuwa alikuwa mjamzito.
Baadhi ya maofisa wa THAT wakipata maelezo kutoka katika familia mojawapo iliyopatwa na matatizo ya kupoteza ndugu kutokana na sababu za kujifungua.

No comments:

Post a Comment