31 July 2013

CHADEMA,CCM WAKABANA KOO



Na Anneth Kagenda
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimesema hakitavunja kikundi chake cha ulinzi maarufu kama Red Brigade labda Jeshi la Polisi litangaze kuvunja kikundi cha Chama Cha Mapinduzi (CCM)maarufu kama Green Guard.Kauli hiyo ilitolewa Dar es Salaam juzi na Mjumbe wa Kamati Kuu Taifa CHADEMA ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, Wakili Mabere Marando wakati akihutubia mkutano wa hadhara, ulioandaliwa na diwani wa chama hicho Kata ya Segerea, Azuri Mwambagi.

Alisema, chama chake kinaunda kikundi cha Red Brigade kwa ajili ya kuwakabili Green Guard wa CCM na wala si polisi au wananchi hivyo kama jeshi linaamua kwamba chama chake kisifanye hivyo basi hata CCM isiwe na kikundi hicho."Serikali pamoja na jeshi lake litangaze kwa umma kwamba hivi sasa linavunja kikundi hicho na sisi tutaacha kuunda cha kwetu na kama hawafanyi, hivyo basi na sisi ni lazima tuwe na kikundi chetu kwa ajili ya kuwakabili vijana hao wa CCM na si polisi wala wananchi,"alisema Mwanasheria huyo.
Alisema, lengo la kuunda vikundi hivyo ni kutokana na kiongozi mkuu wa chama hicho (CCM) kutoa maelekezo ya kuhimarishwa kwa vikundi hivyo ili viweze kutumika nyakati za chaguzi mbalimbali kwa kupiga viongozi wa chama chake na kusema baada ya kuona hivyo alimwagiza Bw. Freeman Mbowe ili kuunda Red Brigade ambayo itakabiliana na Green Guard ya CCM na si polisi.
"Katika hili tunaliambia Jeshi la Polisi kwamba hawa wa kwetu ni kwa ajili ya kukabiliana na kikundi cha chama pinzani na hatupo tayari kuomba radhi kwa lolote lile kwani nasi tunataka kujilinda wenyewe,"alisema.
Alisema, wapende wasipende kikundi hicho kitakuwepo kwani lengo lake ni zuri ambapo ni kwa ajili ya kuwalinda CHADEMA na kukabiliana na kikundi hicho cha CCM ambacho kimekuwa kikinyanyasa viongozi wa chama chake.
Diwani Mwambagi, akihutubia mkutano huo kwa wananchi alisema anaunga mkono kauli ya Wakili Marando na kusema, tofauti na hilo katika mchakato wa kuendelea kuwahudumia wananchi kwa ajili ya kuwaletea maendeleo amekuwa akikumbana na changamoto kubwa kutokana na kwamba hana viongozi wengi wa kusaidiana naye.
"Ndugu zangu wananchi...nyie ndio mlionichagua lakini nimekuwa nikikumbana na changamoto nyingi mara tu ninapoenda kuwatetea mfano kuna suala la barabara ya kilomita 1.6 lakini mita 800 ili ifike Changombe Stendi wamezikatalia lengo lao likiwa ni kutaka kuzitumia kujinadi kwenye uchaguzi ujao kwa kununua kanga na kofia,".
"Hivyo ninawaomba tutakapo takiwa kufanya mabadiliko ninaomba mniunge mkono kwani mita hizi nilazima zirudishwe kwani CCM ni wanyang’anyi na ndio wanaofanya vitendo hivi," alisema Mwambagi.
Hata hivyo, aliwazuia wananchi hao kuwa ni marufuku mwananchi yeyote kutozwa ushuru wakati hawana soko na kwamba awali ilishatangazwa kuwa, kama mtu hana soko hatoruhusiwa kufanya hivyo lakini cha kushangaza wananchi hao wamekuwa wakikubali kutozwa ushuru jambo alilosema ni marufuku hadi hapo soko katika mitaa mitano litakapojengwa.


No comments:

Post a Comment