16 May 2013

Wanafunzi 15 mbaroni kwa kuchoma moto bweni

Na Esther Macha, Mbeya


 WANAFUNZI 15 wa Shule ya Sekondari ya Wazazi ya Lupata wilayani Rungwe, mkoani Mbeya wanashikiliwa na polisi kwa kosa la kuchoma moto bweni wakipinga hatua ya wanafunzi wenzao kusimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya, Diwani Athuman, alisema tukio hilo lilitokea Mei 14, mwaka huu saa 2.00 usiku.
Kamanda Athuman alisema kuwa wanafunzi hao baada ya
kuona wenzao watatu wamesimamishwa masomo walianza kufanya vurugu usiku na kuanza kuchoma moto bweni moja la wanafunzi wa kiume. Kamanda Athuman aliwataja wanafunzi waliosimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu shuleni hapo kuwa ni, Joseph Robert (18), Mwita Chacha na Daniel David (18).
“Hawa wanafunzi watatu waliosimamishwa masomo walihamasisha wenzao kuunga mkono kupinga adhabu hiyo kwa kufanya vurugu na kuchoma bweni hilo,”alisema Kamanda Athuman.
Alisema bweni lililochomwa moto walikuwa wanaishi wanafunzi ambao hawakuwa tayari kuunga mkono uvunjifu huo wa amani shuleni hapo. Aidha Kamanda Athuman alisema wanafunzi 15 wanashikiliwa na polisi wakiwemo vinara wa fujo hizo.
Kuhusu mali zilizoharibiwa, Kamanda huyo alisema thamani halisi ya uharibifu uliotokea bado haijajulikana. Kamanda Athuman ametoa wito kwa jamii hasa wanafunzi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi kwani ni kinyume cha sheria na badala yake watatue matatizo kwa njia ya mazungumzo kwa kufuata mamlaka husika.

No comments:

Post a Comment