27 May 2013

Wafanyabiashara waandamana kupinga ushuru

Na Patrick Mabula, Kahama


 WAFANYABIASHARA wa mazao ya nafaka na wasafirishaji wenye magari malori, wilayani Kahama wameandamana hadi ofisi za Halmashauri ya wilaya wakipinga ushuru wanaotozwa kuwa ni mkubwa.
Wafanyabiashara hao waliandamana juzi na kuvamia ofisi za halmashauri hiyo baada ya malori yaliyokuwa yamebeba nafaka kukamatwa na askari mgambo kutokana na mgogoro huo wakipinga kutozwa ushuru mara mbili.
Kundi hilo la wafanyabiashara wakiwa katika ofisi za Halmashauri hiyo, askari mgambo aliyekuwa akilinda alilazamika kupambana nao bila mafanikio huku akitishia kuwalipua kwa bunduki hali iliyowatia hasira na kusababisha vurugu kubwa.
Wakiongea na waandishi katika ofisi hizo wafanyabishara hao walikuwa
wakipinga kutozwa ushuru mara mbili wa sh. 2,500 kwa kila gunia la mahindi na mpunga wanapoyasafirisha toka vijijini kwa wakulima.
Bw. Imani alisema wao kama wafanyabiashara wamekuwa wakilipa ushuru wa sh.500 kwa kila gunia kwa mzabuni wa halmashauri wanaponunua toka kwa wakulima wanapoanza kuyasafirisha na wamekuwa wakitozwa tena sh. 2,000 hali, ambayo wanapinga.
Mgogoro huo wa ushuru unatokana na kutofautiana katika kikao cha hivi karibuni cha baraza la madiwani na watendaji wa halmashauri, ambapo madiwani walipendekeza ushuru wa mazao uwe sh.1,000 kwa gunia, lakini mkurugenzi alisema wao wamepitisha shilingi 2000.
Katika kikao hicho diwani wa kata ya Lunguya Bw. Benedicto Manwali aliwasilisha pendekezo la Madiwani la kutoza ushuru wa mazao msimu huu sh.1000, lakini lilikataliwa na mkurugenzi, Bi. Isabella Chilumba katika kikao hicho hali iliyopelekea kubaki hivyo hivyo.
Aidha kutokana na mvutano huo ndiyo uliopelekea kuzusha mgogoro huo wa ushuru,ambapo Bw.Manwali alipotafutwa aliitupia lawama Halmashauri kuwa imesababisha hali kutokana na kupinga mapendekezo ya ushuru walioupitisha katika kikao cha ndani cha madiwani wa CCM.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama, Bw. Joseph Gwassa akiongea na wafanyabiashara hao ambao walishinda katika ofisi hizo kutwa nzima alisema suala la mgogoro huo hawezi akalitolea uamuzi peke yake mpaka atakapolifikisha katika vikao vinavyohusika.

No comments:

Post a Comment