MJUMBE wa
Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (MNEC) ambaye pia ni Mwenyekiti wa
Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Tanga, Dkt. Edmund Mndolwa amewataka wananchi wakazi
wa Wilaya ya Korogwe Vijijini kujikita katika kilimo cha alizeti ili kiweze
kuwakomboa kiuchumi.
Dkt. Mndolwa
alieleza kuwa mazingira ya wilaya hiyo na Mkoa wa Tanga kwa ujumla yanahimili
kilimo cha alizeti hivyo kama wananchi watakithamini na kulifanya zao hilo kuwa
la biashara watanufaika haraka kwa kuondokana na umaskini na utegemezi.
Kiongozi huyo
aliyasema hayo wakati akiwahamasisha wananchi kutoka vijiji vya kata na tarafa
za wilaya hiyo juzi na kuwahakikishia wananchi hao kwamba kilimo cha alizeti
hakitawaacha maskini kutokana na utafiti wa kisayansi kuthibitisha ubora na
manufaa ya zao hilo ikiwa ni
pamoja na kuthibitika kuwa na soko kubwa.
"Kwa vile
chama chetu kinahimiza kilimo kwanza, katika ilani chini ya Mwenyekiti na Rais
wetu, Dkt. Jakaya Kikwete, Kamati Kuu ilipitisha uamuzi wa kuwa alizeti ni zao
la biashara katika wilaya yetu na mimi nimeagizwa na chama kuhimiza zao hili
ili muweze kunufaika nalo.
"Lakini kabla ya kufikia hatua
hii ilinibidi nitembelee Kata ya Kwadelo, Kondoa mkoani Dodoma ambayo ni ya
mfano hapa nchini kwa kilimo hicho ili kujifunza namna ya kulima zao hilo hivyo
limeni zao hili ambalo kwa wilaya yetu tutanufaika zaidi kuliko Kondoa, ambao
wanategemea msimu mmoja wa mvua tofauti na sisi tunaopata misimu miwili,"
alieleza.
Akifafanua manufaa makubwa ya zao
hilo, Dkt. Mndolwa alisema kuwa hekari moja inaweza kutoa magunia 12 hadi 18 na
kwa maana hiyo wastani wa hekari moja unaweza kupata lita 300 za mafuta ambazo
ni sawa na thamani ya sh.450,000.
Pia alisema kuwa mkulima akiamua
kulima misimu yote miwili kutokana na hali ya hewa ya wilaya hiyo, atakuwa na
uhakika wa kuingiza sh.900,000 kwa hekari, pato ambalo litawasaidia kupata
mahitaji nuhimu ikiwa ni pamoja na kusomesha watoto na huduma za afya na malazi
kwa familia.
Dkt. Mndolwa alisema mafuta ya zao
hilo ndiyo yenye soko kubwa kwa sasa, hivyo kuwataka wananchi hao kutokuwa na
wasiwasi juu ya upatikanaji wa soko na badala yake waunge mkono kilimo hicho
ili kiweze kuwakomboa kiuchumi.
Katika kuonyesha kwamba anataka
wananchi hao walime alizeti, Dkt. Mndolwa aliahidi kuwalimia vijana ekari tano
kila kata, ambao watajiunga katika vikundi vya watu watano ili kuanza kupata
shamba darasa.
Akitilia mkazo juu ya umuhimu wa
kilimo hicho, Diwani wa Kata ya Kwadelo, Kondoa, mkoani Dodoma, Alhaji Omari
Kariati alisema kuwa wakati wananchi wa kata yake wanaanza kulima zao hilo
hawakuanza na mafanikio ya moja kwa moja lakini kwa sasa wamefanikiwa.
"Kwa sasa mkulima mdogo katika
kata yangu analima ekari 50 na kuna watu wanalima mpaka ekari 200, kitu ambacho
kimefanya wananchi wa Kata ya Kwadelo kutokuwa na shida ya fedha badala yake
wanashindana kimaendeleo.
"Hata vijana na akina mama mkiamua
mnaweza kwani katika kata yetu, kundi lenu ndilo lenye kumiliki uchumi mkubwa
na hawana muda wa kupoteza zaidi ya kuzungumzia namna ya kuboresha kilimo chao
cha alizeti, kitu ambacho mnatakiwa kukifanya pia watu wa Korogwe
Vijijiji," alieleza.
Kariati alisema wakati wanaanza kulima, kata yake
ilikuwa na matrekta matano lakini kutokana na manufaa makubwa ya kilimo hicho
kata ina matrekta 65, ambayo yanamilikiwa na wananchi wenyewe.
No comments:
Post a Comment