30 May 2013

Serikali iangalie upya mfumo ukopeshaji wakulima’

Na Elizabeth Joseph, Dodoma


 WADAU wa kilimo nchini wameitaka Serikali kuuangalia upya mfumo w a k u w a k o p e s h a wakulima pembejeo za kilimo.
Pia wameitaka kuangalia mfumo wa kuwakopesha wakulima kwa kupitia taasisi za kifedha ili ulete manufaa kwa wakulima wadogo nchini.
Hayo yalibainishwa juzi mjini Dodoma na wadau hao katika semina kwa wakuu wa mikoa na wilaya nchini iliyolenga kuutambulisha mfumo mpya wa kuwakopesha wakulima ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa kupitia benki na kuongeza kuwa mfumo huo unaweza kumfanya mkulima mdogo ambaye ndiye mlengwa akashindwa kukopeshwa kutokana na urasimu uliopo katika taasisi hizo za kifedha.
Pia walisema kuwa wakulima wakubwa ndio mara zote wamekuwa wakitumia taasisi hizo kukopa fedha kwa ajili ya kilimo chao hivyo wasije wakajinufaisha wao binafsi kupitia mfumo
huo na kuwasahau wakulima wadogo.
Akizunguma katika mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mwantum Mahiza aliwataka wadau hao kutotanguliza kushindwa kwasababu kila jambo lina changamoto zake na badala yake waende kusimamia mfumo huo kwa umakini ili uweze kuleta tija kwakuwa wananchotaka wakulima ni kuoneshwa njia ya jinsi ya kutumia mfumo huo ili waweze kujiongezea kipato.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Erasto Mbwilo alieleza kuwa mfumo huo unahitaji usimamizi wa karibu kutoka kwa wadau wote wa kilimo ili uweze kufanikiwa kama ulivyokusudiwa.
"Hakuna kitu kinachofanikiwa bila ya kuwa na usimamizi wa karibu na ndiyo maana hata mfumo wa vocha za pembejeo kwenye baadhi ya maeneo ulishindwa kufanikiwa kutokana na kutokuwa na usimamizi makini," alisema Mbwilo.
Awali Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chizza alisema wameamua kuutambulisha mfumo huo kwa wadau ili kupata maoni yao kuhusiana na mfumo huo kabla ya kuanza kuutumia kwa wakulima nchini.
Alibainisha kuwa mfumo wa vocha za pembejeo ulikuwa na changamoto nyingi ikiwemo udanganyifu kwa watu waliopewa dhamana ya kugawa vocha hizo ndio hivyo kuwataka wadau hao kuukubali mfumo huo.
Hata hivyo alibainisha kuwa mfumo huo utakwenda sambamba na vocha za pembejeo hasa kwenye maeneo ambayo yalionesha mafanikio makubwa ya kilimo kwa kutumia mfumo huo.

No comments:

Post a Comment