27 May 2013

Polisi wanusurika kufa wakikimbiza pikipiki

Na Said Hauni, Lindi


 ASKARI wawili wa Jeshi la Polisi akiwemo mmoja wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, wamelazwa katika Hospitali ya Nyangao, baada ya pikipiki waliyokuwa wakiitumia kugongana na gari ndogo.
Ajali hiyo ilitokea wakati askari hao wakimkimbiza mwendesha pikipiki aliyekuwa amekiuka Sheria za Usalama Barabarani. Kamanda wa Polisi mkoani humo, George Mwakajinga, alisema ajali hiyo imetokea wilayani humo Mei 20 mwaka huu.
Aliwataja askari hao kuwa ni F 6986 PC Living aliyevunjika miguu yote miwili na mkono wa kushoto na G 2116 PC Edwin, ambaye amepata maumivu ya ndani kwa ndani.
“Hawa askari walikuwa kazini wakiwa wamepakiana kwenye pikipiki aina ya
Suzuki namba PT 2951, iliyokuwa ikiendeshwa na PC Living, waligongana na gari ndogo aina ya Land Cruiser namba T 398 AME iliyokuwa ikiendeshwa na Bw. Juma Mandundu.
“Ajali hii ilikuwa mbaya na dereva wa gari amejisalimisha mwenyewe Kituo cha Polisi Wilaya ya Nachingwea na atafikishwa mahakamani baada ya taratibu kukamilika,” alisema.
Mashuhuda wa ajali hiyo, wameliambia gazeti hili kuwa, askari hao walikuwa wakiikimbiza pikipiki nyingine ambayo dereva wake alikaidi amri ya kumtaka asimame na kuelekea upande wa Barabara ya Masasi.
Walisema kitendo hicho kiliwafanya askari hao wachukue pikipiki yao na kuanza kumfukuza na walipofika katikati waligongana uso kwa uso na gari ndogo ambalo hawakuliona kutokana na vumbi.

No comments:

Post a Comment