27 May 2013

Mwingine anaswa kwa uchochezi

Na Mwandishi Wetu


 JESHI la Polisi nchini, limeendelea kuwasaka wachochezi wanaotumia simu za mkononi kwa kutuma ujumbe mfupi wa maneno (sms), ili kuhamasisha vurugu.
Operesheni hiyo inafanywa na Kikosi Maalum kutoka Makao Makuu ambao wanasaidiana na Makamanda wa Polisi kwenye mikoa mbalimbali nchini pamoja na wananchi.
 Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana na Msemaji wa jeshi hilo nchini, SSP Advera Senso, alisema tayari jeshi hilo limemkamata mtu mwingine mkoani Lindi kwa kuhusika na uhalifu wa aina hiyo.
“Tayari tumekamilisha upelelezi na kukusanya ushahidi wa mtu aliyekamatwa Dar es Salaam kwa tuhuma za kutuma meseji za uchochezi na leo atafikishwa mahakamani.
“Tunaendelea kukamilisha ukusanyaji ushahidi dhidi ya wanaofadhili ambao
wanashawishi vitendo hivi ili na wao waweze kufikishwa mahakamani mapema,” alisema.
Aliwashukuru wananchi kwa ushirikiano wao wa kutoa taarifa zinazofanikisha operesheni hiyo na kuomba waendelee kuwaunga mkono kwa kutoa taarifa za watu wanaofadhili vitendo vya uhalifu kwa njia ya pesa au ushauri.
SSP Senso alitoa onyo kwa mtu yeyote au kikundi cha watu wanaojihusisha na vitendo vya uchochezi kuacha mara moja kwani watakamatwa bila kujali vyeo vyao au umaarufu wao.

No comments:

Post a Comment