27 May 2013

Pinda afichua siri Mtwara


*ASEMA MAKAMPUNI 45 YAJITOKEZA KUTAKA KUWEKEZA
*KUZINDUA UJENZI KIWANDA CHA SARUJI, AJIRA NJE NJE


Na Mwandishi Wetu, Mtwara


 SERIKALI imesema kuwa, makampuni 45 tayari zimejitokeza na kuomba kuwekeza mkoani Mtwara, baada ya ugunduzi wa gesi asilia kwenye Bahari Kuu Kusini mwa Tanzania.
Makampuni hayo ni pamoja na Dangote Industries ya Alhaj Dangote ya nchini Nigeria inayotaka kuzalisha saruji tani milioni tatu kwa mwaka na kitaajiri wafanyakazi 1,000 ndani ya kiwanda na nje 9,000 ambao ni wakala, wasafirishaji, wajenzi, wauzaji rejareja.
Waziri Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, aliyasema hayo mjini humo jana
kwenye Ibada ya kuwekwa Wakfu Askofu Lucas Mbedule wa Dayosisi mpya ya Kusini Mashariki ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).
“Kesho (leo), nitaweka jiwe la msingi la Kiwanda cha Saruji cha Dangote...viwanda vingine vinavyotarajiwa kujengwa hapa Mtwara ni kile cha mbolea, bidhaa za plastiki na kusindika gesi asilia kwenye mitungi,” alisema Bw. Pinda.
Alisema hivi sasa kuna viwanda vinne vya saruji nchini vyenye uwezo wa kuzalisha tani 3,000 kwa mwaka, ila vinazalisha tani milioni 1.2.
Aliongeza kuwa, Bandari ya Mtwara nayo itapanuliwa pamoja na kujengwa reli ya kuunganisha mkoa huo na machimbo ya chuma yaliyopo kwenye mikoa jirani.
Bw. Pinda alisema ofisi yake ndiyo inayoratibu Kituo cha
Uwekezaji nchini (TIC), ambapo viwanda vitakavyoanzishwa mkoani humo kutokana na ugunduzi wa gesi asilia vitakuwa na manufaa makubwa ya kiuchumi kwa wananchi wa mkoa huo na Taifa kwa ujumla.
Alisema viwanda vyote ambavyo vitajengwa mkoani humo vitakuwa na manufaa makubwa ya kiuchumi kwa wana Mtwara hususan kwenye suala la ajira na kukuza kipato chao.
“Kuhusu tatizo la maji hapa Mtwara, nimemuagiza Waziri wa Maji alete wataalamu waje kuangalia uwezekano wa kupata maji kutoka Mto Ruvuma unaotenganisha Tanzania na Msumbiji,” alisema.
Aliwataka viongozi wa dini watafute mbinu za kuhakikisha Taifa linaongozwa kwa amani ili kuleta maendeleo ya kiuchumi.
Aliahidi kushughulikia maombi ya KKKT kupata ardhi eka 30 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Elimu, wilayani Masasi.
Bw. Pinda aliwasili mkoani humo juzi akitokea mkoani Dodoma kwa ajili ya kushiriki ibada ya kuwekwa Wakfu Askofu Mbedule na uzinduzi wa miradi ya viwanda vitakavyotumia gesi


No comments:

Post a Comment